March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waitara aridhishwa na TBA ujenzi wa miradi

wandishi Wetu, TimesMajira Online

NAIBU Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mwita Waitara ameipongeza Menejimenti ya Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) kwa kazi nzuri wanazozifanya ikiwa ni pamoja na Ujenzi wa miradi mbalimbali ambayo inazingatia viwango vyote vya bora pamoja na kutumia wataalam wa ndani.

Waitara ametoa pongezi hizo alipofanya kikao na viongozi hao pamoja na kufanya ziara ya kutembelea Mradi wa nyumba za Makazi za Magomeni Kota ambapo TBA ni Mkandarasi na Mshauri Elekezi.

Akizungumza katika kikao na Menejimenti ya TBA, Waitara amesema, TBA wamekuwa wakijenga majengo ya kisasa akitolea mfano Ujenzi wa mradi wa jengo la makazi lililopo mtaa wa Simeon Jijini Arusha alilotembelea hivi karibuni ambalo likikamilika litatatua changamoto ya makazi kwa watumishi wa umma.

Katika mradi wa Magomeni Kota Waitara amefurahishwa kwa kazi nzuri iliyofanyika katika mradi huo ikiwa ni pamoja ubunifu wa ziada wa Ujenzi wa vizimba kwa ajili ya wafanya biashara wadogo maarufu kama machinga pamoja na maduka ya kisasa (Shopping Malls) ambayo yatasaidia kutoa huduma kwa wakazi wanaozunguka eneo hilo.

Waitara amesisitiza usimamizi mzuri wa majengo hayo pamoja na kuhakikisha TBA inatoa elimu kwa watakaokuwa wakazi wa nyumba hizo.

Mtendaji Mkuu wa TBA Arch. Daud Kondoro akizungumza katika kikao cha Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mwita Waitara na Menejimenti ya TBA baada ya kufanya ziara kwenye mradi wa Magomeni Kota leo jijini Dar es Salaam. (Na Mpigapicha Wetu)

Mtendaji Mkuu wa TBA Arch. Daud Kondoro amemshukuru Naibu Waziri kwa kutembelea miradi mbalimbali ya TBA na kumuhakikishia kutekeleza maelekezo yote aliyoyatoa katika ziara hizo.