March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wahudumu wa afya ngazi ya jamii wapewa mafunzo ya lishe bora

Judith Ferdinand, Timesmajira Online-Mwanza

Watoa huduma za afya ngazi ya jamii wa Halmashauri  ya Manispaa ya Ilemela, mkoani Mwanza wamepatiwa mafunzo kazini ya lishe bora na umuhimu wa vitamini A na dawa za minyoo kwa watoto wa chini ya miaka mitano.

Hii ikiwa ni njia ya kutambua umuhimu wa lishe kwa mama na mtoto ambayo kimsingi  husaidia kukua vyema kwa mtoto kimwili kuwa na kinga pamoja na nguvu za kupambana na magonjwa hivyo kuharakisha ukuaji wake.

Mafunzo hayo  yametolewa Desemba 11,2025, na Ofisa Lishe wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela,Pili Kassim,ambapo amesema  lengo kuu la mafunzo  hayo ni kuwajengea uwezo na kuongeza ufanisi kwa watoa wahudumu wa afya ngazi ya jamii ili waweze kufanya kazi katika mitaa yao.

“Pia  kuhakikisha huduma za lishe zinafanya vizuri na tunategemea baada ya mafunzo haya huduma za kilishe zitaimarika katika vituo vyetu vya kutolea huduma,” amesema Pili.

Kwa upande  mtoa huduma za afya ngazi ya jamii kutokea Kata ya Kahama,Lukona  Nangulo,amesema mafunzo hayo yamemumwezesha  kutumia kipimo cha utepe (muaki), kupima uzito  kwa ajili ya kutambua hali ya afya ya mtoto.

“Nitafanyia kazi mafunzo niliyopatiwa leo kwa kuwapima watoto ili kutambua wenye udumavu na wasiokuwa na udumavu, na wale watakaokutwa na udumavu nitawashauri mama zao kuwaandalia chakula cha lishe na watakao endelea kuwa na hali hiyo wapelekwe kituo cha afya,”amesema  Lukona.

Naye  mhudumu wa afya ngazi ya jamii kutoka Kata ya Kayenze,. Angelina Sulyu,amesema kupitia mafunzo hayo  yamewaongezea ufahamu kuhusu mambo mbalimbali yanayohusu lishe bora kwa mtoto.

Hivyo  amewashauri wakina mama kutokuwafungia watoto wao ndani bali wawapeleke kwenye vituo vya afya ili waweze kupata huduma na elimu mbalimbali zinazohusu lishe.