September 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wahariri washuhudia mafanikio makubwa kiwanda cha MSD Idofi

Na Reuben Kagaruki, TimesmajiraonlineMakambako

BOHARI ya Dawa (MSD) imeendelea kupata mafanikio makubwa kufuatia maboresho yake ya kiutendaji ambayo yamewezesha mipira ya mikononi (gloves) ambazo zilikuwa zilikuwa zikiagizwa nje ya nchi kuanza kuzalishwa chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.

Mageuzi hayo yanathibitishwa na Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Mavere Tukai, yameshuhudiwa na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari nchini waliokuwa kwenye ziara ya kutembelea na kujionea shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na MSD katika Kanda ya Iringa na Kanda ya Dodoma, wiki iliyopita.

Wakati wa ziara hiyo wahariri hao wa vyombo vya habari walijionea uzalishaji gloves) zinazozalishwa na kiwanda cha MSD Idofi, kilichopo katika Mji wa Makambako, mkoani Njombe kwa teknolojia ya hali ya juu.

Kuanza uzalishaji katika kiwanda hicho ni matokeo ya kuanzishwa kwa Kampuni Tanzu ya MSD Medipham Manufacturing CO LTD, ambayo ndiyo mmiliki wa kiwanda hicho na vingine viwili, ambavyo vipo mbioni kuanza uzalishaji.

Kiwanda hicho kimeanza uzalishaji Februali, mwaka huu ambapo tayari kimezalisha jozi (pear) milioni mbili hadi sasa.

Wahariri wa vyombo vya habari wakielezwa jinsi mipira ya mikononi (gloves) inavyozalishwa katika kiwanda cha MSD Idofi, walipotembelea kiwanda hicho wiki iliyopita.

Akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari, Kaimu Meneja wa kiwanda hicho, Shiwa Mushi, alisema kiwanda hicho kina uwezo wa kuzalisha jozi 10,000 kwa saa

Kwa mujibu wa Mushi, kiwanda hicho kina uwezo wa kuzalisha mipira ya mikono milioni 86.4 kwa mwaka sawa sawa na asilimia 83. 4 ya mahitaji ya nchi.

Mbali na kampuni tanzu hiyo kumiliki kiwanda hicho, inamiliki viwanda vingine viwili ambavyo vipo hatua za mwisho kuanza uzalishaji.

Viwanda hivyo ni kiwanda cha kuzalisha bidhaa za pamba kilichopo Simiyu na Zengereni cha Pwani ambacho kitakuwa kinazalisha dawa

Naye Afisa Uhusiano Mkuu wa MSD, Etty Kusiluka, alisema tayari wanaelekea kuanza kuuza bidhaa kwenye viwanda hivyo. alisema kabla ya kuanzishwa kwa kiwanda hicho, MSD ilikuwa mdau mkubwa wa kununua bidhaa hizo, kuuza na kuzisamba kwa wadau, ikiwemo ni pamoja hosptali, vituo na zanahati kutoka nje ya nchi.

Wahariri wakitembelea kiwanda hicho

Chimbuko la kuanzishwa kwa Kiwanda hicho ni mwaka 2020, ambapo Dunia ilikumbwa na ugonjwa wa COVID 19, hivyo kuathiri upatikanaji na usambazaji wa Dawa na vifaa Tiba duniani na hapa nchini

Hali hiyo iliisukuma Serikali kupitia MSD Kuwa na Mkakati wa kuzalisha vifaa tiba na dawa, ili kujiweka tayari iwapo changamoto kama hiyo itajitokeza ikute nchi imejiandaa kuhudumia wananchi wake kwa kupata dawa na vifaa tiba

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wahariri walipongeza uamuzi wa MSD kuanzisha kiwanda hicho hatua ambayo sasa inafanya MSD kuachana na kuagiza Gloves kutoka nje ya nchi.

Wafanyakazi wa kiwanda cha MSD Idofi wakiendelea na mchakato wa uzalishaji gloves

“Haya ni mageuzi makubwa ndani ya nchi yetu,ukifika pale Idofi ndipo utajua MSD inafanya mambpo makubwa katika nchi yetu kwa ajili ya kulinda afya za Watanzania,” alisema Mhariri wa Jamhuri, Stella Aroan.