May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waathirika wa ajali wapewa salamu za pole

Na Mwandishi Wetu,Timesmajiraonline

NAIBU Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Jumanne Sagini, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Usalama barabarani ametoa salamu za pole kwa Watanzania wote ambao wameathirika na ajali za barabarani zilizotokea Mwaka 2023.

Pole hizo amezitoa wakati alipokuwa katika Maadhimisho ya Wiki ya Nenda kwa Usalama barabarani Mkoa wa Dar es Salaam yaliyofanyika katika Viwanja vya Sigara vilivyopo Chang’ombe wilayani Temeke, Mhe. Sagini alisema kuwa, serikali inatoapole kwa wale wote waliokutwa na kadhia ya ajali na pia tuwaombee kwa Mwenyezi Mungu majeruhi wote wapone haraka ili wapate nafasi ya kuendelea na majukumu ya ujenzi wa Taifa hili.

“Natoa pole pia kwa wale wote waliofikwa na machungu kwa kuondokewa na wapendwa wao kutokana na ajali za barabarani, waliotangulia mbele ya haki kwa ajali, ninawaomba watumiaji wote wa barabara muwe waangalifu muwapo barabarani,”amesema Sagini.

Sagini amezitaka Kamati za Usalama Barabarani na Makamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani na askari wao wote kushirikiana ili kuwa na mipango ya pamoja ya kupambana na madereva wakorofi wasiopenda kutii Sheria na Kanuni za Usalama Barabarani. Ambapo ameitaka  jamii ibadilike na kujijengea utamaduni wa kutii Sheria wenyewe bila kushurutishwa.

“Hapa nasisitiza kwa Wakuu wa Usalama Barabarani kusimamia wenyewe zoezi la uhakiki wa leseni linaloendelea ili mwisho wa siku tubaki na madereva wenye sifa tu na kwa yeyote anayetaka kuingia kwenye fani ya udereva lazima apitie mafunzo yatakayomwezesha kuwa mahiri barabarani,”amesema.

Pia Sagini ameipongeza Kamati zote za Dar es Salaam kwa kuweka mkazo wa kutoa elimu katika shule za Msingi na Sekondari pamoja na makundi mengine yanayotumia barabara hususan kundi la wapanda pikipiki za magurudumu mawili na matatu.

Aidha,Sagini amepongeza Kamati zote kwa kufanikisha kupatikana kwa vitendea kazi ambapo ni magari 10, pikipiki 20 aina ya Boxer na BMW 3, Bajaji 1 na vipima ulevi 15 na reflector jackets 400, raincoats 50 na taa za kuongozea magari 50.