March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Vijiji vipya 34 kunufaika na TASAF Namtumbo

Na Yeremias Ngerangera, TimesMajira Online,Namtumbo

HALMASHAURI ya ilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma imeandikisha wanufaika wapya wa TASAF katika vijiji vipya 34 vya Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo kwa kipindi cha TASAF ya tatu awamu ya pili kuanzia mwez februali- aprili mpaka juni 2021.

Akiongea na waandishi wa habari ofisini kwake hivi karibuni mratibu wa TASAF wa Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo bwana Hyasint Mbiro amesema kuwa kwa kipindi cha Februari,Machi na April mpaka Juni 2021 Halmashauri imefanikiwa kuwaandikisha wanufaika wapya kutoka katika vijiji 34 vya Namtumbo.

Mbiro amesema kuwa katika kipindi hicho kaya 7376 zilitambuliwa kuwa ni kaya maskini lakini kaya 170 hazikuandikishwa kutokana na kutojitokeza katika zoezi la uandikishaji na kuondolewa katika orodha ya kaya ya vijiji husika….

Kwa kipindi hicho pia Mbiro amesema wamefanya kazi ya uhawilishaji fedha ya ruzuku kwa kaya maskini 5,228 katika vijiji 42 vya awali vinavyonufaika na mpango wa ruzuku ya serikali kunusuru kaya maskini.

Jumla ya shilingi 399,814,000 zilipokelewa katika Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo ikiwa 200,284,000 zililipwa Januari – Februari 2021 na shilingi 199,530,000 kwa malipo ya Machi na Aprili 2021.

Solomon Hyera mwandikishaji wa kaya maskini kipindi cha tatu awamu ya pili alisema uandikishaji majina ya kaya maskini ulikuwa unaamriwa na kupatikana kupitia mikutano ya hadhara ya kijiji kwa kuorodheshwa kaya zote za kijiji husika ambazo ni maskini na kisha mwandikishaji kupita kila kaya iliyoorodheshwa kwenye mkutano wa Hadhara kujiridhisha kama kweli ni kaya maskini na kuziandikisha

Zoezi la uandikishaji kaya mpya wilayani Namtumbo lilienda vyema licha ya changamoto iliyopo hivi sasa kaya hizo kulalamikia malipo mara baada ya kuhakikiwa pamoja na kaya zile ambazo wakati wa uhakiki hazikuweza kuhakikiwa zinaomba kuhakikiwa ili ziweze kuingizwa katika mpango wa TASAF ya tatu awamu ya pili.