September 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Tunaondoka Mbulu DC tukiwa tumeridhika-Mnzava

Na Mary Margwe, Timesmajira Online,Mbulu 

Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru  Kitaifa mwaka 2024 Godfrey Mnzava amesema  wanaondoka Halmashauri  ya  Wilaya ya Mbulu wakiwa wameridhika na miradi  7 yenye viwango ambayo walioikagua,kuitembelea,kuifungua na kuweka mawe ya msingi.

” Tunaomba hii miradi iendelee kusimamiwa kikamilifu  ili iweze kukamilika kwa ile ambayo iko katika hatua mbalimbali, lakini kubwa ilindwe na kuitunza,” amefafanua Mnzava.

Hayo ameyasema  Julai 14,2024 wakati alipokua akizungumza kwenye makabidhiano ya Mwenge wa uhuru katika Kijiji cha Guneneda Kata ya Tlawi mbele ya Mkuu wa Wilaya hiyo Veronica Kessy.

Kwa upande  wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu Abubakar Kuul amesema Mwenge wa uhuru ulipokua katika Halmashauri hiyo ulifikia miradi 7 yenye thamani ya bilioni 46.3.

Kuul amesema kati ya miradi hiyo mmoja ulikua ni wa ufunguzi, miradi miwili ya kuwekewa jiwe la msingi, mitatu ya kutembelewa na kuonwa na mmoja wa kukabidhi vifaa vya kufundishia, kujifunzia na michezo kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum.

Aidha Kuul amefafanua kuwa Mwenge ukiwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu umeelimisha na kuueneza ujumbe Mkuu wa Mwenge wa uhuru 2024 usemao” Uhifadhi wa Mazingira na uchaguzi wa Serikali za Mitaa chini ya kauli mbiu isemayo ” Tunza Mazingira na Shiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa ujenzi wa Taifa Endelevu”.