May 3, 2025

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Tanzania yapanda katika viwango vya uhuru wa vyombo vya habari Duniani

Na Mwandishi Wetu,Timesmajira

Tanzania imepiga hatua katika viwango vya kimataifa vya Uhuru wa Vyombo vya Habari, kwa kupanda kutoka nafasi ya 97 mwaka 2024 hadi nafasi ya 95 mwaka 2025.

Kwa mujibu wa Ripoti ya Waandishi wa Habari Wasio na Mipaka (Reporters Without Borders – RSF) iliyotolewa tarehe 2 Mei 2025, licha ya Tanzania kupanda kwa nafasi mbili, alama za jumla zimepungua kidogo kutoka 54.80 mwaka 2024 hadi 53.68 mwaka huu.

Ripoti hiyo inayotolewa kiila mwaka imeonesha kuwa Kupanda kwa nafasi ya Tanzania kunahusishwa na hatua mbalimbali zilizochukuliwa na Serikali pamoja na wadau wa sekta ya habari katika kuboresha mazingira ya kazi kwa waandishi wa habari na kukuza uhuru wa vyombo vya habari.

Miongoni mwa hatua hizo ni pamoja na mapitio ya sheria zinazohusiana na habari, ikiwemo Sheria ya Huduma za Habari ya mwaka 2016, ambapo maboresho yamelenga kuondoa vifungu kandamizi na kuweka mazingira wezeshi kwa wanahabari.

Aidha, hatua nyingine zilizosaidia kupanda ni pamoja na kuimarika kwa mawasiliano kati ya Serikali na vyombo vya habari kupitia majukwaa ya majadiliano ya wazi kumesaidia kujenga uaminifu na kuongeza uwazi katika upatikanaji wa taarifa.

Vilevile, Serikali imeonyesha dhamira ya kulinda haki za msingi kwa raia, ikiwemo haki ya kupata taarifa na uhuru wa kujieleza, hatua iliyosaidia kuboresha taswira ya Tanzania katika jukwaa la kimataifa.

Ripoti ya RSF hutathmini hali ya uhuru wa vyombo vya habari katika nchi 180 kwa kutumia vigezo vitano vikuu ambavyo ni kisiasa, mfumo wa kisheria, mazingira ya kiuchumi, mazingira ya kijamii na usalama wa waandishi wa habari.