September 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Tamasha la utamaduni mkoani Ruvuma lapamba moto, Rais Samia mgeni rasmi

Na Mwandishi Wetu,Timesmajiraonline,Ruvuma

SHAMRA SHAMRA za tamasha la tatu la utamaduni kitaifa litakalofanyika Mkoa wa Ruvuma, zinaendelea kupamba moto, huku Rais Samia Suluhu Hassan akitarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye ufunguzi wake hivi karibuni.

Ufunguzi wa tamasha hilo la tatu la Mkoa wa Ruvuma unatarajiwa kufanyika Septemba 20, mwaka huu na litafanyika kwa muda wa siku nne mpaka Septemba 23, ambapo makabila yataonesha tamaduni mbalimbali.

Wakazi wa Mkoa huo wameonesha shauku kubwa ya kushiriki tamasha hilo ambalo wanalielezea kuwa litakuwa la aina yake kwani mbali na faida zingine litasaidia kuchochea shughuli za kiuchumi za mkoa huo.

Tito Mbilinyi maarufu kama Mwilamu alisema anashukuru sana kwa kuwa ugeni utakaokuja Ruvuma utasababisha manufaa makubwa ya kiuchumi kwa wananchi wa Mkoa huo.

“Hili tamasha sisi wafanyabiashara litatupa manufaa makubwa, kwenye nyumba za kulala wageni, mama lishe, mwenye teksi atanufaika ugeni ni mkubwa watu zaidi ya 5,000 si mchezo, tunawaomba viongozi wa mkoa wetu wawe wanatutengenezea fursa kama hizi,” alisema

“Rais Samia ni msikivu sana anatujali sisi watu wa sekta binafsi kwa sababu zile changamoto ambazo tunakutana nazo tukimwambia huwa anazitatua haraka sana. Tunamshukuru sana na tunamkaribisha sana Ruvuma,” alisema

“Sisi ndio tunajidai kuwa tunalisha mikoa mbalimbai na mataifa mengine yenye uhaba wa chakula. Hili tamasha litatusaidia sana kuinua uchumi wetu wananchi wajitokeze kwa wingi kutumia fursa ya tamasha hili,” alisema

Upendo Hosia ambaye ni mdau wa hoteli mkoani humo, alisema taarifa ya ujio wa Rais Samia wamezipokea kwa furaha sana na watahakikisha wanatumia fursa hiyo kuuwezesha mkoa huo unanufaika kiuchumi.

Alisema uchumi wa Mkoa huo umekuwa ukiimarika siku hadi siku kutokana na kupita magari makubwa ya mizigo yanayochukua shehena ya mizigo kusafirisha maeneo mbalimbali.

“Nikiwa kama mama tunampokea kwa mikono miwili wanawake wa Mkoa huu tumejipanga kumpokea na atafurahi kuona utamaduni wa Mkoa wa Ruvuma, wafanyabiashara na wananchi nawaambia kitu kimoja kwamba ujio huu ni muhimu na fursa kwasababu ugeni huo utaleta maelfu ya watu,” alisema

Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma, Mary Makondo anasema lengo kuu la tamasha hili ni kuonesha na kuhifadhi urithi wa kitamaduni wa makabila mbalimbali ya Tanzania, haswa yale yanayopatikana katika Mkoa wa Ruvuma.

Anasema tamasha hilo linatoa jukwaa kwa jamii kushiriki na kuonesha muziki wa kitamaduni, ngoma, sanaa, mavazi ya kitamaduni, vyakula vya asili, pamoja na mila na desturi za jadi.

Anasema tamasha hili lina umuhimu wa kijamii, kiutamaduni na kiuchumi kwa kuwa linasaidia kuongeza hamasa ya kulinda na kuenzi urithi wa kitamaduni, huku pia likiwavutia watalii wa ndani na nje ya nchi.

Anasema mara nyingi, washiriki kutoka mikoa mingine ya Tanzania na hata kutoka nje ya nchi hushiriki tamasha hili, na hivyo kuleta mchanganyiko wa tamaduni mbalimbali.

Anasema tamasha la Taifa la Utamaduni ni tukio linaloendelea kuimarika na kushamiri nchini Tanzania, likiwa na lengo kuu la kuadhimisha, kuenzi, na kuhifadhi urithi wa kitamaduni wa taifa.

Anasema tamasha hili hufanyika kila mwaka, likiwakutanisha Watanzania kutoka mikoa mbalimbali na wageni wa kimataifa kwa ajili ya kusherehekea tamaduni za asili za nchi. Kwa miaka mingi, tamasha hili limekuwa kiini cha kushirikisha, kujenga na kuimarisha mshikamano wa kitaifa kwa kupitia sanaa na mila za kitamaduni.

***Malengo ya Tamasha la Taifa la Utamaduni

Tamasha la Taifa la Utamaduni lina malengo kadhaa makuu ambayo yamekuwa yakiimarisha umuhimu wake kwa taifa.

Kwanza kabisa, lengo kuu ni kukuza na kuenzi urithi wa kitamaduni wa Tanzania. Katika mazingira ya utandawazi na mabadiliko ya kijamii yanayotokea kwa kasi, tamasha hili linachangia kwa kiasi kikubwa katika kuhakikisha kuwa desturi, mila, na sanaa za asili zinadumishwa. Kwa njia hii, vizazi vijavyo vina nafasi ya kujifunza na kujivunia tamaduni zao.

Pili, tamasha hili linatoa jukwaa kwa wasanii wa ndani kuonyesha kazi zao, ikiwa ni pamoja na ngoma za asili, michezo ya jukwaani, muziki wa kitamaduni, na sanaa nyingine za kiasili kama vile uchongaji, ususi, na uchoraji.

Hii inatoa nafasi kwa wasanii hawa kupanua soko lao na pia kujifunza mbinu mpya kutoka kwa wenzao, hivyo kukuza tasnia ya sanaa nchini.

Zaidi ya hayo, tamasha hili linasaidia kuimarisha umoja wa kitaifa kwa kuwaleta pamoja watu kutoka kabila, dini, na maeneo mbalimbali ya nchi na linaimarisha mshikamano miongoni mwa Watanzania.

Utamaduni ni chombo chenye nguvu kinachoweza kuunganisha jamii, na kupitia tamasha hili, Watanzania wanapata fursa ya kuona na kushiriki katika tamaduni tofauti, hivyo kuongeza uelewa na heshima kwa tofauti zao.

***Maudhui na shughuli za Tamasha

Tamasha la Taifa la Utamaduni linajumuisha shughuli mbalimbali zinazowakilisha utofauti na utajiri wa urithi wa kitamaduni wa Tanzania.

Muziki wa kitamaduni ni sehemu muhimu ya tamasha hili, ambapo vikundi vya muziki kutoka makabila mbalimbali huonyesha ngoma na nyimbo za jadi, zikiambatana na ala za muziki za asili kama vile ngoma, filimbi, na zeze.

Aidha, maonesho ya mavazi ya kitamaduni yanachukua nafasi ya kipekee na makabila tofauti huonesha mavazi yao ya kipekee yanayowakilisha utambulisho wao wa kitamaduni na hiyo husaidia kuhifadhi mitindo ya mavazi ya asili ambayo ina umuhimu mkubwa katika historia ya Tanzania.

Maonyesho ya sanaa za mikono pia ni sehemu muhimu ya tamasha hili kwani wasanii wa kiasili huonyesha kazi zao za mikono kama vile uchongaji wa vinyago, ususi wa vikapu, na uchoraji wa picha za asili. Haya ni maonyesho ya ubunifu wa hali ya juu unaowakilisha ustadi wa wasanii wa kiasili wa Tanzania.

Michezo ya jukwaani pia ni sehemu nyingine maarufu ya tamasha na hizi ni pamoja na maigizo ya hadithi za kale za kitamaduni, michezo ya sarakasi, na michezo ya kuigiza inayojikita katika masuala ya kijamii.

Michezo hii hutoa elimu kwa hadhira juu ya maisha, maadili, na mafunzo ya kitamaduni, huku pia ikiburudisha.

***Umuhimu wa Tamasha kwa Jamii

Tamasha la Taifa la Utamaduni limekuwa na manufaa makubwa kwa jamii ya Kitanzania. Kwanza, linatoajira kwa wasanii na wafanyabiashara wa sanaa za mikono.

Wasanii hupata fursa ya kuuza kazi zao kwa hadhira kubwa, ikiwa ni pamoja na watalii na wageni wa kimataifa wanaoshiriki tamasha na hiyo huchangia kukuza uchumi wa ndani na kusaidia wasanii wa asili kuimarisha mapato yao.

Pili, tamasha hili linasaidia katika kuimarisha utalii wa kiutamaduni nchini na watalii kutoka mataifa mbalimbali huvutiwa na utajiri wa kitamaduni wa Tanzania, hivyo tamasha hili linakuwa kivutio kikubwa kwao.

Utalii wa kiutamaduni unachangia kwa kiasi kikubwa katika mapato ya nchi, na tamasha hili limekuwa na mchango mkubwa katika sekta hiyo.

Aidha, tamasha hili linaimarisha utambulisho wa kitaifa na heshima kwa utamaduni kwani watanzania wanaposhiriki na kushuhudia tamaduni zao mbalimbali, wanapata fursa ya kutambua thamani ya urithi wao na hivyo kuwa na fahari ya kuwa sehemu ya jamii ya Kitanzania.

Tamasha hilo pia husaidia kupunguza migogoro ya kikabila kwa kuhamasisha umoja na mshikamano kupitia kusherehekea utofauti wa tamaduni.

Mwisho——————————