September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TAKUKURU Mwanza yawezesha kukusanywa milioni 290 kodi ya zuio

Na Daud Magesa, Timesmajira Online, Mwanza

Katika kipindi cha Aprili hadi Juni mwaka huu,Halmashauri za Mkoa wa Mwanza zimewezeshwa kukusanya kodi ya zuio, kiasi cha milioni 290.744 na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU),na kuziwasilisha Mamlaka ya Mapato Tanzania(TRA).


Taasisi hiyo imefuatilia na kukagua miradi 17 ya maendeleo, inayogharimu kiasi cha bilioni 6.5,miradi saba inayotekelezwa kwa sh.bilioni 2.098 ilibainika kuwa na kasoro ndogo ndogo.Hivyo inachunguza miradi yenye mapungufu makubwa.

Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Mwanza,James Ruge,leo akitoa taarifa kwa waandishi wa habari,amesema kodi hiyo ya zuio,imekusanywa baada ya taasisi hiyo kupitia uchambuzi wa mifumo ya ukataji na uwasilishaji wa kodi, iliyolenga kuboresha matumizi ya mashine za EFD’s.

Uelewa duni wa sheria ya kodi kwa watoa huduma,ndio sababu ya Halmashauri ilikuwa haikati kodi hiyo ya zuio kutoka kwa watoa huduma, katika manunuzi ya vifaa ili kuiwezesha serikali kukusanya mapato kupitia zabuni mbalimbali.

Pia sababu nyingine ya kutokusanywa kwa kodi ya zuio ni mapungufu ya mikataba ya zabuni,mifumo ya TRA na halmashauri kutosomana.

Pia wamewafikisha mahakamani watumishi 19,wakidaiwa kutumia mapato ya serikali kwa maslahi binafsi na kushindwa kuyawasilisha benki.

Ametoa wito kwa wananchi kushirikiana na taasisi hiyo, kufichua na kuzuia vitendo vya rushwa katika maeneo ya utoaji huduma na miradi ya maendeleo inayotekelezwa.

Aidha Mkuu huyo wa TAKUKURU amesema katika robo ya kwanza ya 2024/25 mkakati uliopo ni kuzuia vitendo vya rushwa katika uchaguzi wa serikali za mitaa kwa kuwafikia wananchi,wadau na makundi mbalimbali kuwaelimisha madhara na makosa ya rushwa katika uchaguzi.

Ruge amesema tayari wameanza na waandishi wa vyombo vya habari, wataendelea na Asasi za Kiraia,Viongozi wa Dini na makundi mbalimbali ya kijamii watafikiwa.