June 23, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Stendi ya mabasi Mbalizi kufungwa taa za mil.5

Na Esther Macha, Timesmajira Online, Mbeya

MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi CCM Taifa (MNEC) Ndele Mwaselela amehaidi kutoa kiasi cha milioni 5 kwa ajili ya ununuzi wa taa kumi za kufunga katika stendi ya mabasi ya Mji Mdogo wa Mbalizi Wilaya ya Mbeya ili iweze kufanya kazi saa 24.

Uamuzi wa Mwaselela unakuja kufuatia ombi la wananchi ambao ni watumiaji wa stendi hiyo ambalo wameliwasilisha kwenye mkutano wa hadhara kuwa wanashindwa kufanya biashara na magari hayalali stendi kutokana na giza wakati wa usiku.

Akizungumza katika mkutano huo Makamu Mwenyekiti wa Stendi ya Mbalizi -Tarafani Martin Ngemela amesema kuwa kwa kipindi kirefu wameomba kuwekewa taa ndani ya stendi hiyo ili kuwapa mwanya wa kufanya kazi saa 24.

“Stendi hii ni kubwa sana,maana inachukua magari kutoka maeneo tofauti ya Mkoa Mbeya na Songwe hivyo tunahitaji kufungiwa taa hapa ili tufanye kazi saa 24 na magari yaanze kulala hapa,”amesema Ngemela

Kutokana na umuhimu huo Mwaselela amesema kuwa kuanzia siku ya Jumanne atatoa milioni tano ili kununua taa kumi ili kufungwa( kuwekwa) kwenye stendi hiyo huku akiomba shirika la umeme Tanesco kumuunga mkono kwa kufunga taa za ukutani yaani ‘Spotlight’ ili kuongeza mwanga zaidi.

Aidha Mwaselela ameagiza mamlaka zinazohusika na usafirishaji, kusimamia zoezi la mabasi ya mikoani kuingia ndani ya stendi badala ya kupakia na kushushia nje ya stendi hiyo.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mbeya ,Wazidi Mahenge amesema katika mpango wa muda mrefu wanakusudia kufanya maboresho makubwa katika stendi hiyo, ikiwa ni pamoja na ujenzi wa vibanda vya kisasa kuzunguka stendi ambao unaweza kuanza mwaka wa fedha 2025-2026.