May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai

Spika azidi kuwabana wabunge CHADEMA

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

SPIKA wa Bunge Job Ndugai, ameendelea kuwasisitizia wabunge wa CHADEMA kurejesha fedha walizolipwa kwa ajili ya kuanzia Mei 1 hadi 17, vinginevyo huo utakuwa ni wizi sawa na wezi mwingine.

Lakini pia amewataka wabunge vijana kulinganisha mambo kuliko kujazwa mambo na viongozi wao na matokeo yake kuamini kwamba kile wanachoambiwa na viongozi wao, ndiyo mwanzo na mwisho.

Spika alitoa kauli hiyo jana wakati akiahirisha Bunge jijini Dodoma.
Aliwataka kulinganisha mambo matano kabla ya kufikia uamuzi
wanaoambiwa na viongozi wao.

Alisema kwa wabunge kuna mambo ya kuangalia, ikiwemo kujua ni jambo gani lenye maslahi ya nchi,  kuangalia jambo hilo kama lina maslahi ya wananchi wake, kuangalia maslahi ya chama kilichomtuma na pia kujiangalia mbunge mwenyewe.

“Wewe hiyo barua ya Mbowe (Freeman) unaona ina mantiki, je hilo jambo limetokana na maamuzi ya vikao au ni amri ya mtu mmoja, bila
kuyalinganisha hayo na kuangalia moja inakula kwako,” alisema Spika
Ndugai.

Alisema wamekuwa wakizunguka nje wakitaka Lockdown, lakini wananchi wengi hawaelewi maana ya hiyo Lockdown.” Lockdown ni rumande ya ndani. Sasa nani anataka kukaa rumande? Na katika nchi nyingine mabunge ndiyo yameishauri Serikali kuweka Lockdown, sisi hatujashauri jambo hilo na Bunge bado lipo tunaweza kuishauri Serikali, lakini Lockdown ni hatari kubwa.”

Alisema wanaoeneza mambo hayo kuwa Bunge kuna mambo fulani, wakati mbunge anakaa bungeni saa 4 kati ya saa 24 za siku nzima, je hayo masaa mengine anakuwa wapi?

Alisema wabunge hao wa CHADEMA aamelipwa tangu tarehe 1 hadi 17,
halafu wakawa watoro. “Naendelea kusisitiza warudishe fedha hizo maana huo ni wizi, warudishe, wakirudisha hakuna maneno,” alisema.

Alisisitiza kwamba lazima zirudi na hazitakatwa sehemu. “Kwa mtu
ambaye amekuwa mtoro siku tano kazini anafukuzwa kazi,  kwa hiyo
inabidi waeleze kwa nini walipwe mshahara wa mwezi wa tano. Mwezi huu wa tano hautaki mchezo mchezo wa namna hiyo,” alisema.

Pia alisema tayari ofisi ya Bunge imeishapata taarifa ya mikopo ya
wabunge kutoka sehemu mbalimbali, hivyo leo watendaji wa ofisi ya
Bunge wataanza kutoa barua kwa wabunge waliopo ili waweze kujua
taarifa zao.

“Kwa wale wasiokuwepo waendelee kukaa kule na mwisho wa mwezi huu waendelee kukaa kule kule, vinginevyo watashangaa yatakayokuja
kuwakuta,” alisema.