September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Shule ya Msingi Bugarama yakabiliwa uhaba madarasa

Na Patrick Mabula,TimesMajira Online. Kahama

WANAFUNZI zaidi 400 walioandikishwa mwaka 2020 wanaosoma darasa la kwanza katika Shule ya Msingi Bugarama Halmashauri ya Msalala wilayani Kahama, wanakabiliwa na uhaba wa vyumba vya madarasa hali inayofanya kusoma kwa zamu na kwa msongamano mkubwa.

Hayo yamesemwa juzi na Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Bugarama, Kubebeka Leonard alisema mbele ya wadau wa sekta ya elimu alipokuwa akipokea msaada wa mifuko ya saruji 200 toka kwao kwa lengo la kupunguza changamoto hiyo kwa watoto wanaosoma shuleni hapo.

Amesema upungufu huo wa vyumba vya madarasa hasa kwa watoto wa darasa la kwanza, hufanya wasome kwa zamu na kwa msongamano mkubwa na kufanya kuwepo kwa usumbufu mkubwa kwa walimu wanaofundisha wanafunzi hao, kunakochangia kushuka kwa kiwango cha elimu.

Mwalimu Leonard amesema Shule ya Msingi Bugarama yenye jumla ya wanafunzi 2,324, wasichana wakiwa 1,187 na wavulana 1,137 na inakabiliwa na upungufu mkubwa wa vyumba vya madarasa vilivyopo ni 18 na vinavyoendelea kujengwa ni vinne na mahitaji halisi ni vyumba 32.

Amesema baada ya Serikali ya awamu ya tano kuhusu sera yake nzuri ya elimu bure, wananchi kwenye vijiji vya Kata ya Bugarama wanaoishi katika mazingira ya uchimbaji wa dhahabu kwenye migodi midogo midogo, wamepata hamasa ya kuwapeleka watoto na kuhakikisha wanapata elimu.