October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Afisa Habari wa shirika lisilokuwa na kiserikali la One Acre Fund ,Dorcas Tinga akizungumza na baadhi ya wakulima waliofika katika banda hilo kwa lengo la kujifunza .

Shirika la One Acre Fund kusaidia Wakulima 66,000 Chokaa yenye rutuba.

Na Esther Macha,TimesMajira,Online,Mbeya

TANI 100 za Chokaa yenye rutuba kwa ajili ya afya ya udongo zinatarajiwa kutolewa kwa wakulima 66,000 katika Mikoa ya Mbeya, Songwe, Njombe, Iringa na Arusha ili kuongeza uzalishaji wa mazao kutoka gunia 10 kwa ekari hadi 20.

Hayo yameelezwa na Afisa Habari wa Shirika la One Acre Fund, Dorcas Tinga wakati akizungumza na wakulima waliotembelea banda hilo wakati wa maonesho ya sikukuu ya nane nane katika viwanja vya John Mwakangale Jijini Mbeya kwa lengo la kujifunza teknolojia mbalimbali za kilimo.

Tinga amesema bidhaa hiyo ya Chokaa itamsaidia mkulima kupata mavuno mengi kwa sababu madini ya (Acid) ambayo yanaongezeka kwenye udongo kutokana na matumizi ya mara kwa mara ya mbolea kuathiri afya ya udongo.

Amesema mkulima akitumia bidhaa ya chokaa itasaidia kushusha madini ya Acid na kuongeza madini ya Calcium na Magnesium ambayo yatasaidia mkulima kupata mavuno mengi.

Amesema tayari bidhaa hiyo ipo na itaanza kutumika katika msimu ujao wa Kilimo na kuwahamasisha wakulima ambao ardhi zao hazizalishi kwa wingi mazao kutumia ili kupata faida.

Ameongeza kuwa malengo ya Shirika hilo ni kuwawezesha wakulima kunufaika na kilimo kwa kuhakikisha wanawezeshwa pembejeo za kilimo na mikopo ya fedha ambazo zitasaidia shughuli zote za kilimo kwa kujiunga kwenye vikundi vya kuanzia watu watano hadi 16.