April 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mgombea Ubunge kwa tiketi ya CCM Jimbo la Ilemela Dkt.Angeline Mabula

Shilingi Bil.13/-kutumika ujenzi soko la kisasa Kirumba

Na Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

UJENZI wa soko la Kisasa la Samaki la Kirumba lililopo Kata ya Kirumba Wilayani Ilemeka mkoani Mwanza unatarajia kugharimu kiasi cha sh.bilioni 13 ikiwa ni mkakati wa Serikali kuwainua wananchi kiuchumi na kuongeza pato la taifa.

Akizungumza na wananchi wa Kata ya Kirumba mgombea Ubunge kwa tiketi ya CCM Jimbo la Ilemela Dkt.Angeline Mabula waliohudhuria mkutano wake wa kampeni kwa ajili ya kuomba kura uliofanyika uwanja wa Bujumbura mtaa wa Kabuhoro , amesema endapo akichaguliwa atahakikisha anasimamia ujenzi wa soko la Kirumba kwa kiwango cha kisasa zaidi kuliko soko la kariakoo.

Mgombea ubunge kwa tiketi ya CCM Jimbo la Ilemela Dkt.Angeline Mabula

“Niwape siri moja tunalo soko letu la Kirumba,soko lile linakwenda kujengwa kwa ghorofa na litakuwa na ukanda wa kufanyia biashara chini ya ardhi,litakuwa bora kuliko lile la Kariakoo, katika kipindi cha miaka mitano tumejenga barabara ya lami kwenye makutano ya barabara ya Makongoro hadi Soko la Samaki la Kirumba ambapo mwanzo haikuwepo,”amesema Dkt.Angeline.

Dkt.Angelibe aliwaomba wananchi hao kukiamini chama chake na kumpigia kura nyingi mgombea wa nafasi ya urais wa chama hicho Dkt.John Magufuli kama shukran kwa namna alivyosaidia utatuzi wa migogoro ya ardhi ya muda mrefu iliyokuwa kero kwa wananchi hao ikiwemo mgogoro wa ardhi Kigoto kati ya Jeshi la Polisi na wananchi.

Pia amesema mgogoro mwingine wa ardhi ni wa Lukobe kati ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na wananchi wa mtaa huo ambapo uthamini umefanyika na wananchi wameanza kulipwa fidia pamoja na mgogoro wa ardhi Nyagunguru Ilemela ambapo wananchi wameanza kulipwa fidia.

Kwa upande wake Meneja Kampeni wa CCM Jimbo la Ilemela Kazungu Idebe amekemea upotoshwaji unaofanywa na baadhi ya wagombea kutoka vyama pinzani na kutoa lugha zisizofaa wakati wakiomba kura kwa wananchi huku akisisitiza kuwa suala la uchaguzi ni hiari ya wananchi kukichagua chama gani na mgombea gani hivyo kuwaomba kufanya siasa safi sanjari na kusisitiza amani na utulivu.