July 1, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Sagini ataka wananchi kutatuliwa migogoro ya ardhi ngazi ya Halmashauri

Na Zena Mohamed,Timesmajiraonline,Dodoma

NAIBU Waziri wa Katiba na Sheria Jumanne Sagini amewataka wataalamu wa sekta ya ardhi nchini katika ngazi za halmashauri kuwasaidia wananchi kutatua matatizo ya ardhi wasiwaache hadi wafike ngazi ya  Wizara.

“Nitoe wito katika eneo hilo tuna viongozi wa serikali ngazi za Mikoa,ngazi ya Wilaya,Wakuu wa Wilaya,Wakuu wa Mikoa Watendaji wengine ,lakini kwenye halmashauri kuna Wakurugenzi,Wenyeviti wa halmashauri,kuna kamati za madiwani za maeneo hayo kwani tusimalize matatizo huko,”amesema Sagini,

Sagini amesema hayo jijini hapa leo,Juni 28,2024 mara baada ya kutembea mabanda ya Wanasheria wanaoendelea kutoa msaada wa Kisheria kwa wananchi katika viwanja vya nyerere Square Mkoani Dodoma yaliyoandaliwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

 Amesema kuwa alipotembelea mabanda hayo  amebaini kuwa licha ya jitihada za Wizara ya Ardhi kuanzisha kliniki Maalum za utatuzi wa Migogoro ya Ardhi na utoaji wa elimu, hadi sasa imeonekana kufikia idadi ndogo ya watu na kufanya tatizo kuendelea kuwepo kwani wanasheria walikuwepo kwenye mabanda hayo wamemueleza kuwa asilimia kubwa ya wananchi wanaokuja kupata msaada wa kisheria hapo wanamatatizo ya ardhi.

Hivyo amesema kuwa Sagini Wizara ya Ardhi ina jukumu kubwa la kuhakikisha kuwa inatoa elimu kwa wananchi na kuepusha kuendelea kushamiri kwa migogoro kama hiyo.

“Tuombe Wizara ya Ardhi, pamoja na kazi nzuri wanayoifanya ikiongozwa na Mheshimiwa Waziri wa Ardhi Jerry Silaa kupunguza Migogoro hii, pia iendelee kutoa elimu na kuelimisha Wananchi kwani tatizo hili bado lipo,”amesema Sagini.

“Kwahiyo nimepitia hapa nikabaini nimepata taarifa fupi zaidi ya watu 150 wamefika hapa wakiwa na matatizo mbalimbali wamesikilizwa na imeonekana kama ilivyoonekana maeneo mengi mengine eneo la ardhi ,migogoro imekuwa mingi na hapa utaona karibu nusu ya watu waliofika hapa msingi wa malalamiko yao ni kwenye sekta ya ardhi,”amesema Sagini

Aidha, ameishukuru ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa maamuzi ambayo yanaonesha Dhamira ya kumuunga Mkono Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ya kuimarisha utoaji wa haki kwa wananchi baada ya kubainika kuwa wengi hawakuwa wanapata au wamenyimwa haki zao.

“Nishukuru kwa Mwanasheria Mkuu wa serikali mwenyewe kwa jambo hili kubwa alilolifanya la kuwa na kliniki ya masuala ya kisheria katika viwanja hivi vya Nyerere Square amefanya jambo linalounga mkono dhamira ya mhe.Rais la kuimarisha utoaji wa haki kwa wananchi .

“Maana yake imebainika katika tume mbalimbali ambazo Rais amezifanya wengi malalamiko yao yanagusa kutopata haki zao kwa wakati au kuhisi kwamba wamenyimwa haki waliyo stahili lakini mengine yanahusa madai,”amesema Sagini

Kwa upande wake ,Mwakilishi wa Chama Cha Mawakili wa Serikali Mkoa wa Dodoma,Odessa Horombe ameeleza kuwa licha ya kupokea malalamiko yanahusu ndoa,mafao lakini  malalamiko mengi waliyopokea hapo kutoka kwa wananchi yanahusu ardhi .

Vilevile amesema kuwa wapo hapo kwajili ya kutoa elimu pia kwani wananchi wengine waliyoifaika katika kliniki hiyo walioneshq kutoyaelewa masuala ya kisheria hivyo wanawapatia elimu.

“Lakini shida nyingine ni elimu tu unakuta wengi wengi hawana elimu kuhusu masuala ya kisheria lakini wakija hapa sisi tunagundua hili ni la kielimu tunamuelimisha anaelewa linaisha,”amesema Odessa.

Kwa upande wa mafao amesema kwamba anaweza akaja mti changamoto ni kuonana na wahusika tu wao wanamkutanisha na wahusika .

“Mtu hajalipwa mafao yake muda mrefu tunamkutanisha na wahusika lakini mengine tunatatua hapahapa kwasababu wanakuja wengine shida ni kuandika tu barua unakuta kaambiwa aandike barua jiji lakini hajui kuandika tunamuandkia anaweka alama ya dole tu,”amesema Odessa.