Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online, Mwanza
Ajali ya moto ambayo chanzo chake akijajulikana kimeteketeza mali ya baadhi ya wafanyabiashara katika soko la mbao la Sabasaba wilayani Ilemela mkoani Mwanza huku Mkuu wa Mkoa huo Said Mtanda,akiagiza uchunguzi kufanyika haraka ili kubaini chanzo cha moto huo.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Mwanza, SSF. Elisa Kamugisha, amesema moto huo ulianza majira ya saa saba usiku kuamkia Machi 17,2025, na walifanikiwa kwa kiasi kikubwa kuuzima mapema ili usienee sehemu nyingine.

“Hapa kuna wafanyabiashara wa mbao zaidi ya 1000,lakini walioathirika na ajali hii ya moto ni 30,lakini taarifa rasmi itatolewa muda siyo mrefu,”amesema SSF. Kamugisha.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Said Mtanda, akizungumza Machi 17,2025, alipowatembelea wafanyabiashara wa mbao katika soko hilo la Sabasaba,ambako ajili ya moto imetokea mbali na kuwapa pole amewataka kuwa watulivu wakati uchunguzi wa chanzo cha moto huo ukiendelea kufanyika.
Mtandao,amesema mara baada ya uchunguzi kukamilika na taarifa kusomwa,ofisi yake itakutana na wafanyabiashara hao pamoja na taasisi za fedha, ili kuona namna ya kuwapa muda zaidi wa marejesho kwa wale waliokopa.
“Natoa rai kwa vyombo vya dola kuharakisha uchunguzi huu ili kutambua chanzo moto,na kujua nini kifanyike na wafanyabiashara hao waendelee na shughuli zao mapema iwezekanavyo kama Serikali inavyohimiza wananchi kuwajibika,”amesema Mtanda.
Sanjari na hayo amewataka wafanyabiashara hao, kuzingatia matumizi ya vifaa vya kuzimia moto na bima, ambayo itawasaidia kuepuka hasara kubwa yanapotokea majanga ya moto kama hilo.
Amesema,mara baada ya kutembelea maeneo yaliyoathirika na moto huo,amepata taarifa kuwa idadi kubwa ya wafanyabiashara hao hawatumii vifaa vya kuzimia moto licha ya elimu ya matumizi hayo kutolewa mara kwa mara na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji.

“Kuna maeneo ya majanga, Serikali inawajibika moja kwa moja kuwagharamia wananchi na mengine haiwajibiki kama hili,nawakumbusha kuzingatia sheria zinavyotaka ili kujihakikishia usalama muda wote wa mali zenu.Jeshi la Zimamoto na Uokoaji mmefanya kazi hii kwa weledi na kuokoa sehemu kubwa ya mali za wafanyabiashara hawa,”amesema Mtanda.

More Stories
PAC yapongeza ujenzi nyumba 109 kwa waathirika wa maporomoko Hanang’
Rais Samia ataka watakao kwamisha huduma za ardhi kuchukuliwa hatua
Kapinga : Ni maono ya Dkt.Samia wananchi wote wapate umeme