September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

RC Mndeme achangia kanisa tani tano za saruji

Na Mwandishi Wetu,TimesMajira Online. Songea

MKUU wa Mkoa wa Ruvuma, Christina Mndeme amewaomba viongozi wa dini kuiombea nchi amani kuelekea Uchaguzi Mkuu unaotarajia kufanyika Oktoba 28 mwaka huu.

Mndeme ameyasema hayo wakati akizungumza kwenye maadhimisho ya kutimiza mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwa Kanisa la Menonite mjini Songea mkoani Ruvuma.

Katika maadhimisho hayo, Mndeme amechangia ujenzi wa kanisa hilo tani tano za saruji zenye thamani ya sh. milioni 1.5.

“Endeleeni kuiombea nchi yetu, tunasali hapa kwa sababu kuna amani, wengine wanakimbia na masanduku na watoto kwa sababu hakuna amani katika nchi zao,” amesisitiza.

Pia amewaomba wananchi wa Mkoa wa Ruvuma na Watanzania kwa ujumla, kuendelea kumuombea Rais Dkt. John Magufuli na wasaidizi wake ili nchi ipate maendeleo zaidi katika sekta mbalimbali.

Kwa upande wake Mchungaji wa Kanisa la Moroviani Usharika wa Songea mjini, Selemani Nzyemba akizungumza kwa niaba ya Mchungaji wa Kanisa la Menonite, amemshukuru Mkuu huyo wa Mkoa na timu yake kwa kwa msaada wa vifaa vya ujenzi.