May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais Samia apongezwa kuwainua wanawake

Na Mwandishi wetu ,Timesmajira online

JUKWAA la Wanawake Kata ya Hananasifu Wilaya ya Kinondoni mkoani Dar es Salaam limempogeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan kwa jitihada mbalimbali alizofanya na anazoendelea kuzifanya nchini kwa ajili ya maendeleo ya wanawake katika nyaja za kijamii na kiuchumi.

Pongezi hizo zimetolewa jijini Dar es salaam katika hafla ya uzinduzi wa jukwaa la Wanawake Kata ya Hananasifu lenye lengo la kuwainua wanawake kiuchumi .

Akisoma risala kwa niaba ya wanawake hao Mwenyekiti wa Jukwaa hilo Alice Taratibu amesema katika kuyafikia maendeleo hayo wanawake kote nchini wameuganishwa katika majukwaa hayo ambayo yamefanikiwa kuwainua kiuchumi.

“Sisi wakina mama wa Kata ya Hananasifu tunampogeza Rais Samia kwa jitihada anazofanya nchini kwa ajili ya maendeleo ya wanawake katika nyaja zote,”amesema Alice

Ameeleza kuwa majukwaa hayo ya wanawake yameundwa kwa mujibu wa mwongozo wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kuanzia ngazi ya Kata,Wilaya, Mkoa na Taifa ambayo lengo kuu ni kujadili fursa za kiuchumi na chagamoto mbalimbali wanazokutana nazo.

Pia amesema Kata ya Hananasifu imefanikiwa kuunda majukwaa ya wanawake katika ngazi za mitaa yote mitano na ngazi ya Kata kukiwa na jumla ya viongozi 30 kutoka katika mitaa na Kata.

“Majukwaa haya yote yanatarajiwa kupatiwa mafunzo maalumu juu ya wajibu na majukumu yao kama viongozi katika mitaa yao ili kuleta chachu ya maendeleo katika familia na taifa kwa ujumla,”amesema.

Nakuongeza kuwa”wakinamama wa Hananasifu wamekuwa wakijishughulisha shughuli mbalimbali za ujasiriamali ikiwemo biashara ndogondogo,ufugaji, ususi, mamalishe pamoja na usindikaji,”.

Vilevile amesema Kata hiyo inajumla ya vikundi 19 vya wanawake wajasiliamali ambavyo vimenufaika na mikopo ya asilimia 10 inayotokana na mapato ya Halmashauri .

Mwenyekiti huyo amesema mbali na mafanikio hayo wamekuwa wakikabiliwa na chagamoto mbalimbali katika kuyafikia maendeleo ya kiuchumi.

Akitaja chagamoto hizo ni pamoja na ukosefu wa elimu ya sheria na haki zake, ukosefu wa mitaji na elimu ya biashara inayoendana na soko la dunia na upatikanaji wa masoko.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Hananasifu Wilfred Nyamwija amewapongeza wanawake wa Kata hiyo kwa kuamua kuunda jukwaa ambalo litakwenda kuwakomboa kiuchumi.

Amesema Serikali imekuwa ikipambana na kuweka nguvu chini ya kuwawezesha wanawake nchini hivyo amewahimiza wanawake kuchagamkia fursa kwani huu ni wakati wao.

“Jukwaa la Wanawake ni fursa kubwa kwenu ya kujitegemea ambayo itawasaidia kuthaminiwa pamoja na kupanda juu na kutimiza ndoto zenu,”amesema. Nyamwija

Pia amewahidi wanawake hao kuwa nao begebega ili kuhakikisha jukwaa hilo linakuwa na tija kwa wanawake katika Kata hiyo.

Aidha aliwaomba wanawake wa Kata hiyo kuendelea kumuunga mkono Rais Dkt Samia Suluhu Hassan Ili waweze kuinuka na kuiinua kata hiyo.