Na Mwandishi wetu,Timesmajira
Mgombea wa Urais chama cha Mapinduzi (CCM) Dkt. Samia Suluhu Hassan siku ya jana amehitimisha kwa kishindo mkutano
wake wa kampeni katika mkoa wa Iringa katika manispaa ya Iringa mjini ambapo amefanya mkutano mkubwa wa hadhara katika uwanja wa mpira wa Samora.
Dkt. Samia aliambatana na viongozi mbalimbali wa kitaifa wa CCM akiwemo Katibu Mkuu Dkt. Asha-Rose Migiro, Katibu wa Itikadi na Uenezi Kenan Kihongosi, wajumbe wa kamati kuu, NEC , viongozi
wa mkoa wilaya na wagombea wa nafasi ya ubunge katika majimbo yote ya Mkoa wa Iringa na nafasi ya udiwani.
Akinadi sera na ahadi zake kwa wananchi waliokuwa wakimsikiza na kumshangilia Dkt. Samia aliwashukuru wananchi na viongozi wa Iringa kwa kujitokeza kwa wingi kumlaki na kumsikiliza Dkt. Samia kabla ya kutoa ahadi mbalimbali amewakumbusha wananchi juu ya miradi mbalimbali iliotekelezwa na serikali yake katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wake.
Mgombea wa Urais ametoa ahadi mbalimbali kwa wananchi na kuwaomba wamchague yeye na wagombea wengine wa CCM ili kuwaletea wananchi wananchi
maendeleo.
KILIMO
Dkt. Samia amewahidi wananchi wa Iringa kuwa endapo atapewa ridhaa ya kuliongoza tena Taifa katika uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka
huu, serikali yake itaendelea kuwekeza katika sekta ya Kilimo ili kuwainua wakulima katika maeneo mbalimbali ya Nchi wakiwemo wa Iringa.
Amesema kuwa katika kipindi kilichopita mkoa wa Iringa ulinufaika na miradi ya kilimo ikiwemo kilimo cha umwagiliaji ambapo wilaya ya Iringa pekee
ilinufaika na miardi mikubwa 9 ya skimu ya umwagiliaji yenye thamani ya Sh. Bilioni 104.4 Iliyowanufaisha wakulima 62,800 katika mkoa wa Iringa.
Dkt. Samia amesema kuwa serikali yake imetekeleza mradi wa umwagiliaji wa Mtula katika halmashauri ya Mafinga kwa thamani ya Sh.Bilioni 566. Katika hatua nyingine mgombea wa Urais Dkt. Samia Suluhu
Hassan amesema kuwa ni sera yake kuwainua wakulima kwa kuwa ndiyo sekta mama inayoajiri watanzania wengi, ndio maana eneo la ruzuku ya pembejeo amelipa uzito unaostahili.
Amesema upatikanaji wa ruzuku ya mbolea umewawezesha wakulima kuongeza uzalishaji wa mazao mbalimbali.

Ameahidi kuwa endapo watamchagua katika uchaguzi mkuu ujao serikali yake itaendelea kutoa ruzuku ya pembejeo kwa wakulima.
Ameahidi vilevile kuwa serikali yake itajenga vituo 50 vya kuhifadhia mazao ya parachichi sambamba na vituo vya kuhifadhia mazao ya mbogamboga,vilevile amewahidi wananchi wa Iringa kuwa endapo atachaguliwa atajenga maghala ya kuhifadhia mazao ya biashara na chakula katika mkoa wa Iringa.
Sambamba na hili Dkt. Samia Suluhu Hassan ameahidi kuwa serikali yake inampango ya kuanzisha vituo vya ukodishaji wa zana za kilimo ili wakulima wapate huduma za kilimo kwa bei nafuu kwa kuwa serikali itatoza nusu ya bei inayotozwa na sekta binafsi. Dkt. Samia ameahidi vilevile kuimarisha ushirika katika wilaya ya Iringa.
UMEME
Kuhusu nishati ya umeme Dkt. Samia amesema kuwa sekta ya nishati ameifanyia mageuzi makubwa ambapo uzalishaji wa umeme umeongezeka kwa kiasi kikubwa, amesema kuwa katika kipindi kifupi cha miaka minne serikali yake imesambaza umeme katika mitaa na vijiji nchi nzima.
Hatua iliobakia sasa ni kumalizia kusambaza umeme katika vitongoji vilivyosalia, amewaahidi wananchi wa Iringa kuwa iwapo watampatia kura za kishindo atahakikisha umeme unafika katika vitongoji vyote nchini vikiwemo vya mkoa wa Iringa.
Sambamba na hili amesema kuwa serikali yake inampango wa kuongeza vyanzo vya uzalishaji wa umeme kutoka iliyopo sasa hadi megawati 8000 ifikapo mwaka 2030.
MIUNDOMBINU
Kuhusu sekta ya ujenzi na uchukuzi Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema serikali yake imefanya jitihada nyingi katika sekta hii muhimu kwa Uchumi wa watu wa Iringa ambapo uwanja wa ndege wa Nduli sehemu kubwa ya ujenzi umekamilika na tiyari huduma kadhaa zinapatikana ikiwemo ndege kutua ikiwemo ndege za shirika la ndege ATCL na mashirika mengine.

Kuhusu kupunguza msongamano katika mji wa Iringa serikali itakamilisha ujenzi wa Barabara ya mchepuko (bypass) ambapo ujenzi upo asilimia 5 na utakamilika katika kipindi cha 2025-2030.
Dkt.Samia amegusia vilevile ujenzi wa Daraja la Kitwiru-Isakalilo ambapo amesema litakamilishwa katika kipindi kijacho cha awamu ya uongozi wake. Pia aligusia ya kwamba amepokea maombi mengi yaliyootolewa na wagombea ubunge hasa ya ujenzi wa Barabara za lami ambapo amesema amezichukua na atazifanyia kazi katika kipindi cha pili cha uongozi wake.
WAFANYABISHARA NDOGONDOGO
Dkt.Samia amegusia maono yake ya kuinua sekta ndogo ya biashara ambapo katika kipindi cha siku 100 ya uongozi wake sekta hii inajumuisha mama lishe, maafisa usafirishaji (bodaboda) atairasimisha.
Ameahidi kujenga jengo la kisasa la Machinga complex katika mji wa Iringa ili kuwawezesha wafanyabiashara ndogondogo kufanya biashara zao katika mazingira mazuri ili kukuza vipato na biashara zao.

VIWANDA NA BIASHARA
Kuhusu sekta muhimu Samia amesema kuwa licha ya ongezeko la viwanda katika mkoa wa Iringa kutoka 24 mwaka 2020 hadi 40 mwaka , serikali yake itapochaguliwa itahakikisha inajenga kongani ya viwanda katika wilaya ya Iringa ili kuongeza ajira kwa vijana sambamba na kuongeza thamani ya mazao ya kilimo , misitu na madini kwa uchache.
Baada ya kumaliza kwa mafanikio mkutano mkubwa wa hadhara katika manispaa ya Iringa mgombea wa Urais wa CCM, Dkt. Samia Suluhu amefanya mkutano mkubwa wa hadhara katika eneo la Mlowa katika jimbo la Mvumi katika wilaya ya Chamwino mkoa wa Dodoma.
Akiwahutubia mamia kwa maelfu ya wananchi amewaahidi kuwaletea maendeleo iwapo atachaguliwa kulitumikia taifa katika kipindi cha pili katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika mwezi oktoba mwaka huu 2025.
ELIMU
Kuhusu sekta elimu Dkt Samia Suluhu Hassan ameahidi kuwa serikali ikipata ridhaa tena ataendelea kuboresha sekta ya elimu ikiwemo elimu bila ada na kwa ubora. Pia alitanabaisha kwamba iwapo CCM ikichaguliwa itajenga shule za sekondari katika Kata tatu ambazo hazina shule.
Ameahidi kujenga shule ya sekondari yenye kidato cha tano na sita katika jimbo la Mvumi mkoani Dodoma.
MAJI
Akijibu maombi yaliyotolewa na mgombea ubunge jimbo la Mvumi ndg liivingstone Lusinde kuhusu kutibu maji yenye chumvi katika jimbo la mvumi Dkt Samia ameahidi kulishughulikia jambo hilo kwa uzito unaostahili kwa kuwaleta wataalam ili kuyapima maji ili yaweze kufaa kwa matumizi ya binadamu katika kipindi kijacho cha uongozi wake.

More Stories
TUCASA yaomba kuanzishwa sheria malipo sekta ya ujenzi
Kihongosi:Uhai wa chama mashina
Kihongosi: Msigombane kwa itikadi za vyama