September 23, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais Samia aanza ziara Ruvuma leo

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwasili katika uwanja wa Ndege wa Songea kwa ajili ya kuanza ziara ya kikazi Mkoani Ruvuma tarehe 23 Septemba, 2024.

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online

RAIS Samia Suluhu Hassan, leo Jumatatu ameanza ziara ya kikazi Mkoani Ruvuma ambayo ataihitimisha siku ya tarehe 28 mwezi huu.

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Ahmed Abbas Ahmed, amewaambia waandishi wa habari kuwa Rais Samia akiwa mkoani humo atafanya mambo makubwa matatu ambayo ni kufunga tamasha la tatu la taifa la utamaduni linalomalizika leo na kufanya ziara ya kikazi kuanzia tarehe 24 mpaka 28.

Amesema Rais atazitembelea wilaya tano za Mkoa wa Ruvuma ambapo ataongea na wananchi wa Mkoa huo kupitia mikutano ya hadhara na atazindua na kuweka mawe ya msingi kwenye miradi mbalimbali ya mandeleo iliyoko mkoani humo.

RC amesema Rais Samia pia atashiriki mkutano wa Umoja wa Wanawake wa Chama cha Mapinduzi CCM Taifa litakalofanyika wilayani Songea na atafunga kikao hicho tarehe 28 Septemba na kuhitimisha ziara yake siku hiyo ambayo pia ataongea na wananchi katika uwanja wa Maji Maji.

“Nawakaribisha wananchi waje kwenye mkutano wa tarehe 28 atakapohitimisha ziara yake na nawakaribisha waandishi wote wa habari kwa namna ya kipekee washiriki ziara ya mheshimiwa Rais kuanzia mwanzo mpaka mwisho na siku atakapoondoka mkoani hapa tarehe 29 tujitokeze kumshangikiwa kwa ziara yake,” amesema

Wakati huo huo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Pindi Chana alizungumza na machifu wa mkoa wa Ruvuma na kuwataka kuendeleza mila na utamaduni kwa kuwarithisha kizazi cha sasa na kizazi kijacho.

Amewaambia machifu hao kuwa Tanzania inautulivu na amani kutokana na kazi kubwa inayofanywa na viongozi wa dini na machifu wa makabila mbalimbali.

“Mila na desturi muendeleze, leo hii nchi yetu watu hawaulizani dini wala kabila na hiyo ni kutokana na kazi kubwa iliyofanywa na viongozi wa dini na machifu kwa hiyo mnawajibu wa kuendeleza kurithisha,” amesema