September 22, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Pwani wakunwa kasi ya Rais Samia ukarabati barabara zilizoathiriwa mafuriko

Na Mwandishi wetu,Timesmajiraonline, Pwani

MIONGOZI vya mambo ambayo yanafanya wananchi kuwa na mvuto mkubwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, ni kwa jinsi inavyowapelekea maendeleo wananchi.

Lakini kubwa zaidi ni kwa jinsi inavyokimbilia wananchi pale wanapopatwa na majanga mabalimbali kama ambavyo tumekuwa tukishuhudia kwa nyakati tofauti.

Mfano, yalivyotokea maafa yaliyosababishwa na maporomoko ya tope, mawe na visiki, wilayani Hanang, mkoani Manyara kilichofanywa na Serikali kimeongeza imani ya wananchi kwa Rais Samia.

Hiyo ni kwa sababu Serikali ilichukua hatua za haraka kuhakikisha wananchi wanaendelea na maisha yao ya kawaida na wote tumekuwa mashuhuda wa hilo.

Lakini pia wakati wa mafuriko ya hivi karibuni yaliyotokea mkoani Pwani na kukata mawasiliano ya barabara, kazi kubwa iliyofanya na Serikali wote tumeona.

Mbali na Serikali kutoa misaada ya kibinadamu, tumeshuhudia jitihada ambazo Serikali imechukua kurejesha katika hali ya kawaida miundombinu ya barabara iliyoharibiwa kutokana na mafuriko hayo.

Miaka ya nyuma tulishuhudia wananchi wakilalamika kwa Serikali kushindwa kutimiza wajibu wake kwa wakati pale yalipotokea majanga, kama vile wakati wa tetemeko la ardhi mkoani Kagera, lakini malalamiko hayo kwa sasa hayapo.

Mfano, hivi karibuni Naibu Katibu Mkuu (Miundombinu) kutoka Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Injinia Rogatus Mativila, alifanya ziara na kukagua ujenzi wa barabara mkoani Pwani, ambazo ziliathiriwa na mafuriko.

Alijionea barabara ambazo zinatakiwa kufanyiwa marekebisho zikiendelea kujengwa, huku wananchi wakiridhisgwa na hatua mbalimbali zinazochukuliwa.

Akizungumza na wananchi , Mhandisi Mtavila anasema Serikali imejipanga vizuri kuhakikisha inafanya maboresho ya kudumu kwenye barabara kwa kuzifanyia matengenezo.

“Pamoja na kuziwekea lami barabara za Mkoa wa Mpwani, ni lazima wasimamizi wa miradi hiyo kuhakikisha barabara hizo zinajengwa kwa viwango vilivyowekwa kwa manufaa ya wananchi,” anasema mhandisi Mativila na kuongeza;

“Hapa Utete ambapo ujenzi unaendelea vizuri tumesisitiza barabara ijengwe kwa ubora na kumalizika kwa wakati kwa manufaa ya wananchi, lakini pia ipo barabara ya kilometa 32 ambayo inachanganywa udongo na kemiko na hii inakaa muda mrefu.”

“Lakini hatukuishia hapo katika kuhakikisha Serikali chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan inatimiza mahitaji yake kwa wananchi, tumekuja hapa Muhoro, kutembelea daraja linalounganisha kwa kilomita 32 na hili usawa wake utakuwa mkubwa kwenda juu ili maji au mafuriko yasivuke kwenda maeneo mengine, kwani tunatarajia kuwekwe tuta moja kwenda juu.”.

Mhandisi Mativila, anasema tayari mkandarasi amepewa maelekezo kuwa wanataka daraja lenye ubora ambalo hata baada ya kumalizika litakaa muda mredu sana bila kuleta tatizo lolote.

Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini- Tanzania (TARURA) mkoani Pwani, Mhandidi Leopard Runji, anashukuru kwa ujio wa kiongozi huyo na kusema anaamini lengo kuu la Serikali ni kutatua kero za wananchi linatimia, kwani Serikali imekuwa ikiweka nguvu kubwa kwa kuhakikisha inatatua kero za wananchi wake ili kuwaletea maendeleo.

Anasema daraja la Muhoro ambalo awali lilikuwa linajaa maji, hivi sasa limepata ufumbuzi wa kina, kwani wanaamini baada ya matengenezo hayo kumalizika wananchi wataendelea kuishi kwa amani, wakiendelea kutumia barabara zao bila matatizo na kwa muda mrefu.

“Tunaipongeza sana Serikali yetu kupitia Rais Samia, kwani anafanya kazi mzuri, amejitaidi kuhakikisha wananchi wanapata maendeleo makubwa katika nyanja tofauti kwa ajili ya maendeleo wa Watanzania wote,” anasema Injinia Runji na kuongeza;

“Lakini pia shukrani zetu za pekee ziende kwa Naibu katibu mkuu kututembelea na kuona jitiada tunazoendelea nazo na pia tunamwakikishia kuwa maelekezo yote aliyotupatia tutayafanyia kazi bila kupepesa macho na kuhakikisha kila kitu kinaenda kilivyopangwa kwa wakati na kwa ubora kwa manufaa ya wananchi,”.

Baadhi ya wananchi walioshuhudia ugeni wa viongozi hao katika maeneo mbalimbali ya ujenzi wa miundombinu hiyo walipongeza sana uamuzi wa Serikali ya kurejesha miundombinu iliyoharibiwa na mvua kwa haraka na kwa wakati.

Wanasema kwamba wanaamini kinachofanyika hakina Serikali ya Rais Samia masihala badala yake Serikali imejipanga kuwakwamua wananchi kutoka kwenye madhara yaliyosababishwa na mafuriko.

Wanasema wanaridhishwa na kazi ya ujenzi wa barabara za mkoa wa Pwani, hivyo wanaona jinsi kodi zao zinavyofanyakazi.