October 9, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Profesa Mkenda kufungua maonesho ya elimu, utafiti na ubunifu

Khadija Bagasha, Timesmajira Online,Tanga

Maonesho ya elimu, utafiti na ubunifu kitaifa yanafanyika mkoani Tanga ambayo yanafunguliwa Leo Mei 27, mwaka huu na Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda.

Huku yakitarajiwa kufungwa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Mei 31,mwaka huu ambayo yanayohusisha taasisi za elimu, utafiti na ubunifu zaidi ya 300 yanayofanyika katika viwanja vya Popatlal jijini Tanga.

Mkuu wa Wilaya ya Tanga James Kaji amewakaribisha wananchi wa Mkoa Tanga kwenye maonesho hayo kwa siku zote hizo kwani yatatoa nafasi ya watu kupata elimu kupitia nyanja mbalimbali sambamba na fursa zilizopo zinazotokana na taasisi zinazoshiriki.

“Zipo taasisi mbalimbali bunifu ambazo zinaweza kutupa elimu ikiwemo Sido kwa kujua namna gani tunaweza kuongeza thamani ya mazao tuliyonayo, tuna matunda je tutapata ujuzi katika usindikaji wa matunda tukianzia katika vikundi wenzetu walioendelea kama China na India ni viwanda vidogo vidogo ndio vilivyowanyanyua badala ya kutegemea viwanda vikubwa, “amesisitiza Kaji na kuongeza kuwa;,

“Ni nafasi ya pekee kwa vikundi vya uzalishaji katika mazao mbalimbali ikiwemo matunda kuja kupata elimu ya bure kwa taasisi za ubunifu ili kuweza kuinua mazao yetu tuliyokuwa nayo,”.

Aidha Kaji amesema kuwa vyuo vikuu vyote nchini vitakuwepo kwenye maonesho hayo ikiwemo taasisi za elimu na ubunifu hivyo wakazi wa Mkoa wa Tanga watumie fursa hiyo kuwapeleka watoto wao ikiwemo kuchukua fomu za kujiunga na vyuo mbalimbali nchini.

“Tuna bodi ya mikopo hapa lakini tuna vyuo vya ufundi, kwaio ni nafasi ya pekee kwa wananchi wa Tanga muje kupata maelekezo ya namna ya kuanzisha vyuo,mmekuwa na vilio vingi sana kwenye mitandao kuwa hamna vyuo vikuu bahati sasa imekuja sasa njooni muulize maswali mupate elimu ya kutosha,”.

Baadhi ya wadau walishiriki kwenye maonesho hayo wakiwemo Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) wamesema ushiriki wao kwenye maonyesho hayo utawawezesha kujifunza mambo mapya lakini na jamii pia itajifunza nini wanachokifanya.

Mkurugenzi wa Shahada za Awali Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) Dkt.Hamis Haji Salum amesema wameshiriki kwenye maonesho hayo kwa lengo la kuonesha miradi mbalimbali inayofanywa na wanafunzi wao ambazo zina ubunifu wa kutumia teknolojia ya habari.

Akizungumzia teknolojia hizo hususani Smart Poultry Farm inayohusiana na masuala ya mifugo kujua namna gani ya kufuga kwenye njia ambayo ni nzuri kwa mfano “tumezoea watu wanavyofuga kizamani lakini sasa tumekuja na teknolojia mpya ya kufuga,”.

Mradi mwingine ni wa Smart west been mradi unaoelezea jinsi gani ya uhifadhi wa mazingira kwa mfano”kila mmoja anapiga kelele kuhusu mazingira yawe safi na salama lakini bado wanaendelea kutupa taka ndio maana tunakuja na njia nzuri ya utunzaji wa mazingira ili takataka hizo zisiweze kuleta madhara,”amesema Dkt.Salum

Mradi mwingine ni wa watoto njiti wanaozaliwa chini ya muda wao ambao wapo katika kitengo cha ICU ambapo teknolojia hiyo ina uwezo maalumu wa kudhibit joto, unyevunyevu na vitu vingine kama vile harufu yenye madhara kwa mtoto.