September 23, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

PPRA yasajili wafanyabiashara katika mfumo wa NeST

Na Jackline Martin, TimesMajira Online

Mamlaka ya udhibiti ununuzi wa Umma Nchini (PPRA) imefanikiwa kusajili wafanyabiashara watano katika mfumo wa NeST na kuwahudumia wateja zaidi ya 76 huku ikiwataka wafanyabiashara kuendelea kuchangamkia fursa za zabuni serikalini ili waweze kukuza uchumi wa Tanzania

Akizungumza na waandishi wa Habari Agosti 21, Mwaka huu Wakati wa Tamasha la Kariakoo Festival lililofanyika Jijini Dar es  Salaam, Meneja Kanda ya Pwani kutoka Mamlaka ya udhibiti Ununuzi wa umma nchini (PPRA)-Vicky Mollel,alisema Serikali imetenga fursa mbalimbali kwaajili ya kukuza uchumi wa watu pamoja na kampuni za kitanzania ikiwemo kutenga kazi za mpaka Bilioni 50 ili ziweze kufanywa na watanzania.

“Tangu maonesho yaanze tunashukuru muitikio wa wafanyabiashara umekuwa mkubwa kwasababu wapo ambao wametembelea katika banda letu kwasababu wamesikia katika matangazo kwamba PPRA wapo katika eneo hili lakini kwa ajili ya kuwaelimisha”

“Wapo ambao wamekuja wamepata elimu na baada ya kupata elimu wameweza kujisajili katika mfumo na mpaka kufikia leo tumeweza kufanya usajili wa wafanyabiashara watano na tumeweza kuhudumia wateja zaidi ya 76 n wameomba tuweze kuwatembelea katika ofisi zao na hiyo tumechukua kama changamoto kwamba wakati mwingine tunaweza kuamua kupita kwenye maduka ili kuwaelimisha kwasababu wafanyabiashara ni wengi lakini wengine hawafahamu hizi fursa zilizopo serikalini” Alisema na kuongeza kuwa

“Kwa niaba ya mkurugenzi mkuu wa PPRA Denis Simba kwa wafanyabiashara mbalimbali ni kwamba wachangamkie fursa za zabuni/tenda serikalini ambazo zipo kwaajili yao na kwa sasahivi tayari serikali au taasisi nunuzi zimeshatangaza mpango wa ununuzi kupitia mfumo wa NeST kwahiyo watakapoingia kwenye ukurasa wa mbele kwenye mfumo huo wanaweza kuona kazi mbalimbali ambazo zimetangazwa na taasisi nunuzi ni wajibu wao sasa kwenda kuzichangamkia fursa hizo kwenda kuziangalua fursa hizo na kuziomba fursa hizo ili tuweze kukuza uchumi wetu kama Tanzania” 



Mollel alisema wametumia
Maonesho hayo kwaajili ya kutoa elimu kwa wafanyabiashara mbalimbali kuhusiana na masuala ya matumizi ya mfumo wa NeST, kuwaelimisha wafanyabiashara fursa mbalimbali lakini pia kuwaelimisha wafanyabiashara fursa mbalimbali za zabuni zilizopo serikalini.

“Kama PPRA tumeshiriki katika maeneo haya ili kuweza kuwafikia wafanyabiashara mbalimbali kwaajili ya kuwafundisha fursa zilizopo pamoja na kuweza kuwasajili katika mfumo wa NeSt”



Kwa upande wake Afisa ununuzi Mwandamizi wa Mamlaka ya udhibiti wa ununuzi wa Umma,  Emmanuel Kelia alisema kutokana na serikali kuipa jukumu Mamlaka hiyo kusimamia na kufatilia taasisi nunuzi, wameanzisha ofisi mbalimbali za Kanda kwa lengo
La kusogeza huduma hizo karibu na wanufaika

“Miongoni mwa ofisi zetu za Kanda tulizonazo ni ofisi ya Kanda ya Pwani  inayohudumia mikoa ya Dar es salaam, Morogoro na Pwani, pia ofisi za Nyanda za juu kusini inayohudumia mikoa ya Mbeya, Iringa, Njombe pamoja na Songwe, aidha tuna ofisi za Mamlaka zilizopo Nyanda za Kusini inayohudumia Mkoa wa Mtwara, Songea na Lindi , pia tuna ofisi za Nyanda za Kaskazini inayohudumia mkoa wa Arusha, Kilimanjaro, Manyara pamoja na Tanga na ofisi za Kanda ya Ziwa inayohudumia mkoa wa mwanza, Kagera, Simiyu, Mara na Shinyanga lakini pia tuna ofisi katika Kanda ya magharibi inayohudumia
mkoa wa Tabora, Katavi na Kigoma, maeneo Mengine ya Dodoma na Singida ynahudumiwa na Ofisi ya Makao makuu iliyopo Dodoma”