September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Polisi yawatoa hofu wanaofungua maduka yao

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online, Mwanza

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza laendelea kuwahakikishia hali ya usalama wafanyabiashara waliofungua maduka yao nakuendelea na kazi kwa kuongeza doria mtaani.

Ambapo wafanyabiashara ambao wameanza kufungua maduka wamehimizwa wafungue kwa sababu hawatafanyiwa kitu chochote kibaya na mtu yeyote kwani Jeshi hilo ndivyo lilivyojipanga hivyo kusiwe na visingizio vyovyote vya kukosa usalama katika Mkoa huo.

Mapema Juni 26, 2024 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Wilbrod Mutafungwa akiwa kwenye doria amefika mtaa wa Lumumba na kuzungumza na baadhi ya wananchi na wafanyabiashara wa eneo hilo na kuwaondolea hofu ya kiusalama wale wote waliofungua maduka yao.

“Mtu anafunga duka lake eti anaogopa mtu mwingine kumfanyia fujo asifanye biashara yake vizuri, doria yetu imelenga kuwaondolea hofu ya aina yoyote kama Mkoa ulivyokuwa salama, sisi Jeshi la Polisi tunaendelea kujipanga kwa kuongeza askari watakaokuwa kwenye doria za magari, za miguu na pikipiki,” amesema Kamanda Mutafungwa.

Aidha Mutafungwa amewataka wafanyabiashara wanaotishiwa wasifungue maduka yao watoe taarifa Polisi ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa kwa haraka.