May 1, 2025

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali yaboreshwa kuleta tija upatikanaji haki

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

SERIKALI imesema,katika kuimarisha upatikanaji haki na utawala bora, Serikali kupitia  Sheria ya Marekebisho ya Sheria za Sekta ya  Sheria, Namba 11 ya 2023 ilifanya marekebisho ya  muundo wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa  Serikali kwa kuanzisha Ofisi ya Mwandishi Mkuu  wa Sheria.

Waziri wa Katiba na Sheria Dkt.Damasi Ndumbaro ameyasema hayo Leo Aprili 30,2025 Bungeni jijini Dodoma wakati akiwasilisha bajeti ya Wizara yake kwa mwaka wa fedha 2025/2026.

Alisema lengo la maboresho hayo ni kuongeza  tija na ufanisi katika shughuli za uandishi wa  sheria, urekebu na ufasiri wa sheria.

Kwa mujibu wa Dkt.Ndumbaro,muundo wa  kiutawala wa Ofisi hiyo  uliidhinishwa na Rais wa  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mnamo 14  Januari, 2025 ili kuiwezesha kuendelea kutekeleza  majukumu yake.

Aidha alisema , tayari Ofisi imepewa fungu la kibajeti ambalo ni Fungu 101 kwa ajili ya  kuiwezesha Ofisi hiyo kuandaa Mpango na Bajeti  kila mwaka. 

Vile vile alisema,Wizara kupitia Ofisi  ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (OMMS)  imeendelea kuhakikisha kuwa sheria za nchi  zinakwenda na wakati na zinaakisi sera na  vipaumbele vya Serikali katika nyanja za kisiasa,  kiuchumi, kijamii, kiutamaduni, kimazingira na  kiteknolojia.

Dkt.Ndumbaro alisema,katika kipindi cha Julai, 2024 hadi Aprili, 2025 Ofisi iliandaa Miswada ya sheria 16.

Alieleza kuwa katika kipidi hicho, Wizara kupitia OMMS ilisimamia  utangazaji wa Sheria Kuu mpya 15 ambazo  zilisainiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano  wa Tanzania na kutangazwa kwenye Gazeti la  Serikali .

Kwa mujibu wa Dkt.Ndumbaro,katika kipindi cha  Julai, 2024 hadi Aprili, 2025, Wizara kupitia Ofisi  ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ilihakiki na  kuchapisha jumla ya Sheria Ndogo 903, ikilinganishwa na Sheria Ndogo 885 zilizohakikiwa na  kuchapishwa katika kipindi kama hicho Mwaka  2023/2024.

“Lengo la kutengenezwa kwa sheria  ndogo ni kufafanua maudhui yaliyobainishwa  kwenye Sheria Kuu. Sheria hizo zinajumuisha Kanuni  125, Amri 171, Notisi 408, Sheria Ndogo 182, Matamko tisa na Hati nane.

Pia alisema ,katika mwaka 2024/2025, jumla ya Sheria Ndogo Kifani  40 ziliandaliwa kwa ajili ya kuziongoza Wizara, Taasisi  na Mamlaka za Serikali za Mitaa katika uandaaji  wa Sheria Ndogo.

“Sheria zilizoandaliwnajumuisha Sheria 32 za Wizara na Taasisi za Serikali na nane  za Halmashauri,aidha, Sheria Ndogo Kifani  zinaandaliwa kwa ajili ya kuingizwa katika Mfumo  wa kielektroniki wa OAGMIS ili kupunguza dosari  za uandishi pamoja na kurahisisha mchakato wa  uhakiki. “alisisitiza

Alilieleza Bunge kuwa kati ya Sheria hizo, Sheria nane zimekamilika na zimewekwa kwenye Mfumo wa  OAGMIS baada ya kuhakikiwa na kuanza  kutumika  01 Machi, 2025.

Katika hatua nyingine Waziri huyo alisema,katika kutekeleza  programu ya kutumia lugha ya Kiswahili kwenye  utoaji haki na kuwawezesha wananchi kuzielewa  Sheria za nchi, Serikali imeendelea kuhakikisha  kuwa Sheria zote za nchi zinapatikana katika lugha  ya Kiswahili na Kiingereza.

Alisema huo ni utekelezaji wa  Sheria ya Tafsiri ya Sheria Sura ya kwanza mapitio ya  Mwaka 2021 inayoelekeza kutafsiri sheria zote  zilizopo katika lugha ya Kiingereza kuwa katika lugha ya Kiswahili.

Hivyo alisema, katika kipindi cha Julai,  2024 hadi Aprili, 2025,

Wizara kupitia Ofisi ya  Mwanasheria Mkuu wa Serikali imekamilisha  uhakiki wa mwisho wa Sheria Kuu 300 kati ya 446zilizotafsiriwa kwa lugha ya Kiswahili. Dkt.

Dkt.Ndumbaro       alisema,katika        kuhakikisha  kuwa sheria zote za nchi zinaendana na wakati na  kuwarahisishia watumiaji katika kufanya rejea ya  sheria husika hususan wakati wa utoaji wa haki na utekelezaji wa wajibu ikiwemo huduma za kimahakama na ukusanyaji mapato, Wizara kupitia Ofisi ya  Mwanasheria Mkuu wa Serikali imekamilisha  urekebu wa Sheria Kuu 446 za nchi na kuandaa  Toleo la Sheria Zilizofanyiwa Urekebu la Mwaka  2023.

“Zoezi hili limefanyika kwa mujibu wa Sheria  ya Urekebu wa Sheria, Sura ya nne toleo hili ni la pili  tangu Nchi yetu ilipopata uhuru.

“Aidha, kwa  kuzingatia uzito na umuhimu wa urekebu wa  sheria, Toleo hili lilizinduliwa na  Dkt. Samia , kwa hafla maalum iliyofanyika tarehe 23  Aprili, 2025 Ikulu-Chamwino. Toleo hili litaanza  kutumika tarehe 1 Julai, 2025.

“Hatua hii ni  sehemu ya jitahada za Serikali ya Awamu ya Sita  katika kuimarisha utawala bora, utawala wa sheria  na kuimarisha misingi ya utoaji haki. 

Vilevile alisema,Wizara kupitia Ofisi  ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, imeendelea  kushiriki na kutoa ushauri wa kisheria katika  majadiliano mbalimbali ya mikataba ya kibishara,  mikutano ya kitaifa, kikanda na kimataifa.

Alisema,katika  kipindi cha Julai, 2024 hadi Aprili, 2025 jumla ya  Mikataba ya Kitaifa na Kimataifa 2,574 kutoka  Wizara, Idara zinazojitegemea, Mashirika ya  Umma, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ilifanyiwa upekuzi ikilinganishwa na Mikataba 1,280  iliyofanyiwa upekuzi katika kipindi kama hicho  mwaka 2023/2024 sawa na ongezeko la asilimia  101.

Dkt.Ndumbaro alisema,ongezeko hili linatokana na juhudi za Serikali  kuongeza idadi ya miradi kwa ajili ya kutoa  huduma kwa wananchi na miradi inayofadhiliwa na  Wadau wa Maendeleo.

 Aidha alisema, Hati za Makubaliano 514 zilifanyiwa upekuzi katika kipindi husika ikilinganishwa na 341 zilizofanyiwa upekuzi katika  kipindi kama hicho mwaka 2023/2024. Alisema,ongezeko  hili linaakisi jitihada za Serikali kuhamasisha  uwekezaji na diplomasia ya ushirikiano wa kikanda  na kimataifa.