September 24, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

NHIF sasa kutoa huduma za afya kwa namba ya NIDA

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

BIMA ya Afya ya Taifa imeanza kutoa huduma kwa wanachama wake kwa kutumia kadi au namba ya kitambulisho cha Taifa (NIDA) ili kurahisisha upatikanaji wa huduma za afya kwa wanachama wa mfuko huo.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye maonesho ya wakulima na wafugaji (88) kwenye viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma Kaimu Meneja kitengo cha Mawasiliano NHIF Grace Michael amesema hatua hiyo inakwenda kumrahisishia mteja kupata huduma za afya hata kama kadi ameisahau nyumbani.

Amesema hatua hiyo imekuja kutokana na mfuko wa NHIF kuendelea kuimarisha mifumo yake ya utambuzi wa wanachama wake hasa wanapokuwa katika vituo vya kutolea huduma za afya.

Michael amesema ,kwa sasa mwanachama anaweza akatambuliwa kituoni kwa kutumia namba ya NIDA .

“Hii inakwenda kuondoa changamoto ya wateja kukosa huduma za afya kwa kusahau nyumbani au kuwapoteza  kadi ya NHIF. “Amesema

Hata hivyo amesema,kwa wanaopoteza kadi hizo wanapaswa kufuata utaratibu kwenye Mamlaka husika ya kuonesha na kuthibitisha kuwa kadi imepotea.

Ametumia nafasi hiyo kuwaasa wanachama wa mfuko huo na wananchi kwa ujumla kutumia ofisi za NHIF  ajili ya kuuhisha taarifa zao za NIDA huku akisema kwa kipindi hiki kazi hiyo pia inafanywa katika viwanja vya 88 Nzuguni jijini Dodoma.

Aidha amesema,katika kipindi hiki cha maonesho pia NHIF inashughulikia changamoto mbalimbali za wanachama na kuwataka wanachama na wananchi kutembelea banda la NHIF NHIF ajili ya kupata huduma hizo.