October 9, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

NEMC yatilia mkazo wawekezaji kufanya kaguzi binafsi athari za mazingira

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limewataka wenye miradi ya maendeleo kufanya kaguzi binafsi kila mwaka baada ya kupata cheti cha mazingira ili kujitathiimini mwenendo wa uendeshaji mradi na utekelezaji wa masharti ya cheti hicho.

Hayo yamesemwa jijini Dar es Salaam na Meneja wa NEMC – Kanda ya Temeke Arnold Mapinduzi wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na hatua zinazofuata baada ya mwenye mradi wa maendeleo kupata cheti cha mazingira ambapo moja ya masharti ni kufanya ukaguzi binafsi kila mwaka na kuwasilisha taarifa kwa baraza.

Mapinduzi amesisitiza wenye miradi kujikagua na kuwasilisha taarifa sahihi kwa Baraza ili zipitiwe na kutoa ushauri sawia utakaowezesha kuepuka athari zinazoweza kujitokeza kwa wawekezaji wenyewe na kwa jamii.

Naye, Meneja Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma Irene John amesisitiza kuwa baraza litaendelea kutoa elimu juu ya umuhimu wa kaguzi binafsi za mazingira baada ya kuanza kwa mradi ili kulinda viumbe hai na mazingira kwa vizazi vya sasa na vijavyo hivyo kuwezesha maendeleo endelevu ya jamii na taifa kwa ujumla.