April 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mwenge wa Uhuru wapitisha miradi yote Iramba

Na Dotto Mwaibale, TimesMajira Online,Iramba.

MWENGE wa Uhuru ambao umemaliza mbio zake za kukagua miradi ya maendeleo wilayani Iramba mkoani Singida leo na kukabidhiwa Wilaya ya Mkalama umeridhishwa na miradi yote huku Mkuu wa wilaya hiyo akimwagiwa sifa.

Mwonekano wa Tanki la maji la mradi huo.

Baadhi ya miradi iliyopitishwa ni mradi mkubwa wa maji uliopo katika Kijiji cha Kyalosangi Kata ya Kinampanda ambao ulizinduliwa na Mkimbiza Mwenge wa Uhuru Kitaifa Luteni Josephine Mwambashi ambaye aliongozana na Mkuu wa wilaya ya Iramba Suleiman Mwenda na viongozi wengine.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Luteni Josephine Mwambash akipanda mti wakati Mwenge huo  ukiwa katika wilaya hiyo

Mradi huo mkubwa wenye tanki la lita 50,000 kwenye mnara wa mita 6, ujenzi wa vituo vya kuchotea maji 5 umegharimu Sh. Milioni 150, 589, 732.72 na umeongeza upatikanaji wa maji kwa asilimia 1.98 na kufikia asilimia 61 wilayani Iramba.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge Kitaifa Luteni Josephine Mwambashi ametembelea pia chanzo cha mradi huo na kuridhishwa na mradi huo na kuufungua “Tumeona kuna kisima na tumepanda kwenye tanki tumeshuhudia kuna maji, tumeona pia nyaraka ziko vizuri na tumeona mabomba na vituo vya kuchotea maji na wananchi wanapata huduma ya maji hivyo nauzindua mradi huu na sasa nakata utepe ” amesema Mwambashi.

Mkuu wa wilaya ya Iramba Suleiman Mwenda akipanda mti wakati Mwenge wa Uhuru ukiwa katika wilaya hiyo.

Mwambashi amempongeza Mkuu wa Wilaya hiyo Suleiman Mwenda kwa kusimamia vizuri fedha za Serikali katika kutekeleza miradi hiyo yote yenye manufaa makubwa kwa wananchi.