October 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Muwasa yaendelea kusambaza maji kwa Wananchi

Fresha Kinasa, TimesMajira be Online, Musoma.

MAMLAKA ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Musoma (MUWASA) inaendelea na jukumu la usambazaji wa maji ya bomba kwenye Kata za Etaro, Nyegina, Nyakatende na Ifulifu zilizopo wilayani Musoma.

Lengo ni kuhakikisha Wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama karibu na makazi yao ili waondokane na changamoto ya kutembea umbali mrefu.

Hayo yamebainishwa kupitia taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini Juni 5, 2024,ambayo imeeleza kuwa uamuzi wa Serikali wa kusambaza maji ya bomba kwenda kwenye kata hizo nne kutoka chanzo cha maji ya Musoma Mjini Bukanga imelipa jukumu hilo MUWASA.

Baadhi ya hizo kata, zitasambaziwa maji kutoka kwenye bomba kuu la Mugango-Kiabakari-Butiama huku kijiji cha Nyasaungu, Kata ya Ifulifu kimeanza kutumia maji ya bomba kutoka Mugango.

Jesca Adamu ni Mkazi wa Kata ya Nyegina akizungumza na TimesMajira amesema kuwa, upatikanaji wa huduma ya maji Safi na salama unapokuwa karibu na makazi ya Wananchi inasaidia kina mama kushiriki katika shughuli za maendeleo badala ya kutumia muda mwingi kutafuta maji umbali mrefu.