May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Msikiti mpya wa Muhammad wa sita kuanza kuswaliwa na waislamu wote wa Tanzania

Na Mwandishi wetu Timesmajira online

MFALME wa Morocco Mohammed wa sita, ameridhia kuanza kutumika kwa msikiti mpya wa Makao makuu wa Muhammad wa sita kuanza kuswaliwa na waislamu wote wa Tanzania.

Kutokana na Mfalme huyo kuridhia Mufti wa Tanzania Dkt, Sheikh Abubakar Zubeir amewataka waislamu wote kujitokeza kesho kwa ajili ya kuswali swala ya ijumaa ambayo itakwenda sambamba na ufunguzi mdogo wa msikiti huo uliopo Kinondoni Jijini Dar es salaam .

Akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar es salaam leo Msemaji wa Mufti Tanzania ambaye pia Katibu wa Balaza la Ulamaa Sheikh Hassan Chizenga amesema msikiti huo ulikuwa ufuguliwe mapema miaka miwili iliyopita na kueleza kuchelewa huko kumetokana na janga kubwa la Corona ambalo liliikumba dunia .

Amesema janga la Corona liliweka ugumu kwa Mfalme wa Morocco Mohammed wa sita kushidwa kuhudhuria nchini Tanzania kwa ajili ya kuufungua msikiti huo.

” Kutokana na sababu ya Janga la Corona na kusababisha kurefuka kwa mda tangu msikiti kuisha na kwa sababu ya ombi letu waislamiu nchini ambalo lilifikishwa rasmi kwa Mfalme wa Morocco na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan Mfalme wa Morocco Muhammed wa sita ameruhusu kufanyika kwa ufunguzi mdogo ili msikiti huu uanze kutumika”amesema Sheikh Chizenga

Amesema msikiti huo ulijengwa na Mfalme wa Morocco kama zawadi kwa waislamiu wote wa Tanzania.

“Hatua ya kujengwa kwa msikiti huu ilifikiwa baada ya juhudi za viongozi wa kuu wa nchi katika awamu mbili zilizopita ya Rais wa awamu ya nne Dkt Jakaya Kikwete, pamoja na Hayati Dkt John Magufuli kujenga daraja zuri la mawasiliano na Morocco, hatimaye Mfalme akaitembelea nchi yetu na akafikishiwa ombi Hilo”amesema Sheikh Chizenga

Sheikh Chizenga alibainisha kuwa ufunguzi kamili wa msikiti huo utafanyika badae kwa kufuguliwa rasmi na Mfalme mwenye utukufu Muhammad wa sita siku za usoni pale mazingira na mipango ya tukio hilo itakapo kamilika.

Aidha amesema ufunguzi mdogo wa msikiti huo utaanza majira ya saa nne asubuh hivyo aliwataka waislamiu kujitokeza kwa wingi zaidi.