*Kamati ya Bunge uwekezaji wa mitaji ya umma yataka mradi ukamilike kwa wakati
*Wakazi 450,000 kunufaika na mradi
Judith Ferdinand, Timesmajira Online,Mwanza
Utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa matenki matano ya maji yenye ujazo wa lita milioni 31, umefika asilimia 15,ambayo yanajengwa katika maeneo Kisesa,Buhongwa,Usagara, Fumagila na Nyamazobe.
Huku Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma(PIC),imeiagiza Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Mwanza(MWAUWASA), kuhakikisha mradi wa huo unakamilika kwa wakati ili kutatua changamoto ya hupatikanaji wa maji kwa wananchi.

Hayo yameelezwa Machi 21,2025 na Mwenyekiti wa PIC Vuma Augustine, wakati wa ziara ya Kamati hiyo ya kutembelea mradi wa ujenzi wa matenki matano ya maji na kituo cha kusukuma maji eneo la Sahwa,wilayani Nyamagana mkoani Mwanza.
Vuma amesema, baada ya Serikali kujenga chanzo cha maji Butimba, sasa inafanya kazi ya kusambaza maji kwa wananchi ndio maana imeanza utekelezaji wa ujenzi wa matenki hayo ili maji yaweze kuwafikia.
“Tunaamini mradi huu utaenda kuwa suluhisho la hupatikanaji wa maji jijini Mwanza,na dhamira ya kumtua ndoo mama kichwani itakuwa imefanikiwa.Rai yetu MWAUWASA itaendelea kumsimamia Mkandarasi ili tupate mradi bora na ukamilike kwa wakati ili tija yake ifanyike na miundombinu italindwa kwa matumizi ya leo na kesho,”amesema Vuma.
Kaimu Mkurugenzi wa MWAUWASA Neli Msuya, amesema kutokana na changamoto ya maji,walilazimika kuandaa mradi maalumu wa kuboresha usambazaji wa maji ambao ni ujenzi wa matenki matano.
Matenki hayo yatakua ujazo wa lita milioni 31 kwa gharama za bilioni 46.2, kwa ufadhili wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikishirikiana na Shirika la Maendeleo la Ufaransa.Ambapo mkataba ulisainiwa Juni 13,2024 na utekelezaji wake ulianza rasmi Desemba 24,2024 na utakamilika Desemba 24,2026, na Mkandarasi amelipwa kianzio bilioni 8.6.
Neli amesema,mradi huo utahusisha ujenzi wa vituo viwili vya kusukuma maji na mabomba makuu ya kusafirisha maji,kutoka katika vituo vya kusukuma maji kwenda kwenye matenki,ambao kwa kiasi kikubwa unatekelezwa Wilaya ya Nyamagana na kiasi kidogo Magu na Misungwi.
“Wakazi 450,000,watanufaika baada ya mradi kukamilika ni wa maeneo ya Buhongwa, Nyamazobe,Nyahingi,Luchelele,Lh’wahima,Sahwa,Fumagila,Kishiri na Igoma kwa Wilaya ya Nyamagana,Wilaya ya Magu ni Bujora,Kisesa na Kanyama huku Wilaya Misungwi ni Usagara,”amesema Neli.

Kwa upande wake Meneja Miradi wa MWAUWASA, Celestine Mahubi,amesema tenki la maji linalojengwa Sahwa katika kituo cha usambazaji maji litakuwa na uwezo wa kubeba maji lita milioni 3, ambalo litasambaza maji kwenye matenki ya Kisesa Nyamazobe, Fumagila na Usagara.
“Nina imani mradi huu utakamilika kwa wakati kwani utekelezaji kwa sasa upo asilimia 15 lakini muda ambao Mkandarasi ametumia ni asilimia 12 ya muda uliopangwa na kabla ya kuanza mradi huo tuliwashirikisha wananchi,”amesema.
Mmoja wa wananchi wa Mtaa wa Sahwa,Mpemba Babugejeshi,amesema awali walikuwa wanafuata maji maeneo ya mito na walikuwa wanapata ahueni mvua zinaponyesha,lakini baada ya kuja kwa mradi huo wameanza kuota maji kwenye magati ingawa bado changamoto ya upatikanaji maji ipo katika maeneo hayo.
“Tunaimani mradi unavyozidi kuendelea na ukikamilika utatusaidia kutatua changamoto ya maji,hivyo tunaomba ukamilike kwa wakati ingawa tenki la kwanza lilivyokamilika tulipata ahueni ya maji kupitia magati ingawa nayo hayatoshi,”.

More Stories
Dkt. Kazungu: Wizara ya Nishati itaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya Kimkakati.
TFS yapanda Miti 1,500 Kuadhimisha Siku ya Misitu Duniani Tabora
Tanzania na China kushirikiana fursa za TEHAMA kwa wanawake