October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, Mwalimu Commercial Banki, Herman Kessy, (katikati) akifafanua baadhi ya hoja. Kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Bodi Ambrose Nshala na kushoto ni Afisa Mtendaji Mkuu (CEO) wa Mwalimu Commercial Banki Plc. Richard Makungwa.

Mkutano Mkuu Mwalimu Bank, Walimu waambiwa “rudini nyumbani tukuze chetu”

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Tabora.

BENKI ya Mwalimu (Mwalimu Commercial Bank Plc) imewahimiza wanahisa wake wakubwa na wadogo na wananchi kwa ujumla kutumia huduma za benki hiyo kwani inazidi kuimarisha miundo mbinu yake ili kuwafikia wateja kwa urahisi zaidi nchi nzima.

Afisa Mtendaji Mkuu (CEO) wa Mwalimu Commercial Banki Plc. Richard Makungwa akizungumza wakati wa mkutano mkuu wa nne wa wanahisa wa benki hiyo kwenye ukumbi wa Isike Mwanakiyungi mkoani Tabora Agosti 13, 2020.

Akizungumza katika ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 4 wa Wanahisa wa benki hiyo katika ukumbi wa Isike Mwanakiyungi mkoani Tabora Agosti 13, 2020, Afisa Mtendaji Mkuu (CEO) wa Benki hiyo Richard Makungwa amesema benki itaendelea kuimarisha miundo mbinu yake ili kuweka mazingira mazuri ya biashara ambapo hadi hivi sasa licha ya kuwa na matawi mawili ya Dar es Salaam, Benki ipo mbioni kufungua tawi la 3 jijini Dodoma kabla ya mwisho wa mwaka huu wa 2020.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, Mwalimu Commercial Banki, Herman Kessy, akizungumza kwenye mkutano wa nne wa wanahisa wa benki hiyo kwenye ukumbi wa Isike Mwanakiyungi mkoani Tabora

“Tuna huduma za Mwalimu Mobile kupitia *150*31#, vile vile huduma ya Mwalimu Wakala (mpaka sasa tuna mawakala wapatao 90 wanaopatikana nchi nzima). Wateja wetu wanaweza pata huduma za ATM kupitia UMOJA Switch na wanaweza kuweka hela kupitia matawi yote ya TPB Bank nchi nzima. Vilevile tunatarajia kuanza kutoa VISA Card kwa wateja wetu kabla ya kufikia mwishoni mwa mwaka huu.” Richard Makungwa, Afisa Mtendaji Mkuu Mwalimu Commercial Bank.

Amesema Benki itaweka mazingira mazuri ya biashara ili walimu binafsi wanahisa kwa ujumla kutumia huduma za Benki hiyo katika kukata bima za mali na maisha yao kupitia Benki ya Mwalimu ambayo sasa ni wakala wa bima.

Amesema kwa kufanya hivyo Wanahisa wote kwa ujumla wahamasike kutumia huduma za benki hiyo katika kufanyia shughuli zao zote za kifedha kuiwezesha Benki kujiongezea mapato ili kuharakisha muda wa kutoa gawio kwa wanahisa.

Mwanahisa akitoa maoni yake wakati wa mkutano huo

“Benki pia inategemea mapato kutoka katika miamala mbalimbali kama kutoa pesa kwenye akaunti, kutuma fedha kupitia simu vile vile kutuma pesa kwa mfumo wa kibenki (mf. TISS/EFT) na huduma za kibenki kupitia mawakala wetu.” Alisisitiz Afisa Mkuu Mtendaji.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) Bw. Deus Seif. Amesema…“Walimu naomba tutumie benki yetu…tutumie benki yetu, kuna sehemu tulizembea kidogo, wakati viongozi wetu wa Chama Cha Walimu wanaanzisha hii benki waliamini kwamba benki itakuwa na nguvu kuliko mabenki yote kwasababu waliamini walimu wasiopungua 217,000 walioko kwenye pay roll ya Januari 2015 wote watafungua akaunti na kuitumia benki yao na inamaan sasahivi ingekuwa benki kubwa na yenye nguvu, pamoja na changamoto zote hizi lakini tujitahidi kutumia benki yetu.”

Akisisitiza kuhusu umuhimu wa ushiriki wa dhati wa walimu katika benki hiyo Rais wa CWT, Mwl. Leah Ulaya alifafanua kuwa  “Mimi kama kiongozi wa walimu hapa Tanzania nitumie nafasi hii kwanza kuwapongeza kwa maamuzi tuliyofikia leo lakini pia niendelee kuwasihi na kuwaomba wanahisa wenzangu ambao ni walimu tuendelee kuona umuhimu wa kuendelea kuithamini benki yetu na kadiri bodi yetu itakavyotuelekeza wakati utakapofika tupeleke mishahara yetu kwenye benki ya Mwalimu tusisite kufanya hivyo

Awali Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Benki hiyo, Bw. Herman Mark Kessy amesema Mkutano huo wa wanahisa ni muhimu sana kwa sababu pamoja na kupata taarifa rasmi kuhusu mwenendo na utendaji wa Benki, pia umetoa nafasi ya kujadili mambo mbalimbali na kuyafanyia maamuzi.

Baadhi ya walimu ambao ni wanahisa wa Mwalimu Commercial Bank wakifuatilia mkutano mkuu wa nne wa wanahisa wa benki hiyo uliofanyika Agosti 13, 2020 kwenye ukumbi wa Isike Mwanakiyungi mjini Tabora. Rais wa Chama Cha Walimu Tanzania Mwl. Leah Ulaya amewahimiza walimu kote nchini kuithamini benki hiyo na kwamba watumie huduma za benki kwa kupitishia mishahara yao kwenye benki yao.

“Nichukue fursa hii kuwashukuru sana tena sana kwa kuniamini, mimi ninaamini hii benki inakwenda kufanya vizuri sana, kama mkiangalia katika benki zilizoko hapa nchini Mwalimu Commercial benki ndiyo benki ya wazalendo halisi…benki hii ndiyo yenye wanahisa wengi zaidi kuliko benki nyingine yeyote ile ina wanahisa 217,000 katika benki zote zilizo kwenye orodha ya soko la hisa la Dar es Salaam.” Herman Kessy, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Mwalimu Commercial Bank