Fresha Kinasa, TimesMajiraOnline ,Mara.
MKURUGENZI wa Shirika lisilokuwa la Kiserikali linalojishughulisha na kupambana na Ukatili wa Kijinsia Mkoa wa Mara la ‘Hope for Girls and Women in Tanzania’ (HGWT) Rhobi Samwelly amesema Jamii inao wajibu wa kuhakikisha mila na desturi zisizofaa ambazo zimekuwa zinakwamisha Watoto wa kike kushindwa kuendelea na masomo zinapigwa vita.
Amesema, serikali imeendelea kuweka mazingira mazuri na kufanya Uwekezaji mkubwa katika sekta ya Elimu ikiwemo kujenga vyumba vya madarasa vya kutosha, kuajiri Walimu na kuondoa ada ili Watoto wote wapate fursa ya elimu bila vikwazo.
Hivyo, mila ambazo zinawafanya Watoto wa kike wasisome lazima zikemewe na kila mmoja kwa nafasi yake na juhudi za pamoja ziendelee kuchukuliwa baina ya wazazi, Mashirika binafsi na Serikali ili zisikwamishe ndoto zao hasa maeneo ya Vijijini ambako elimu inahitajika zaidi kutolewa.
Rhobi ameyasema hayo Machi 29, 2025 katika Mahafali ya Wahitimu wa kidato cha sita ya Wanafunzi Vijana Wakatoliki Tanzania (TYCS) wa Tarime Sekondari na Ingwe Sekondari yaliyofanyika kwa pamoja shuleni hapo. Ambapo pia amewataka Wahitimu hao baada ya kufanya mitihani ya kidato cha sita, wasijiunge na makundi maovu ama kushiriki matukio ya kihalifu.
“Tuendelee kukemea ukeketaji kwa Watoto wa kike na ndoa za utotoni ambazo zimekuwa zikiwafanya wasitimize masomo yao. Tuwasomeshe Watoto wa kike kwa juhudi zote, tuwalinde na kuwawekea mazingira wezeshi ili wasipate vikwazo. Serikali inataka kuona kila mtoto Mtanzania anasoma tusiwaozeshe watoto wa kike kwa lengo la kupata ng’ombe, tuwapeni urithi wa kudumu ambao ni elimu.” amesema Rhobi.
Pia, ametoa wito kwa Watanzania, kuendelea kudumisha amani, umoja, upendo na mshikamano na kutoshiriki kuvuruga amani iliyopo nchini kwani ndio Msingi wa Maendeleo ambayo yanafanywa na Serikali na kupelekea Taifa kupiga hatua.
Akisoma risala ya Wahitimu hao wa kidato cha sita wa (TYCS) Johnson Joseph amesema kuwa, wanamshukuru Mungu kwani wameweza kushirikiana kitaaluma na wanafunzi wengine katika masuala ya kitaaluma na kuimarisha Umoja.
“Mafanikio mengine tumeweza kununua Vitendea kaz vya kiroho,kuhudhuria makongamano ya kiimani, kujenga ushirikiano kati yetu na Jamii, kuwa na kwaya imara katika tawi letu, kusaidiana kitaaluma, kukuza ufaulu wa wanachama, kufanya matendo mbalimbali ya huruma kwa Jamii ikiwemo,”amesema na kuongeza kuwa.
Mkuu wa shule ya Tarime Sekondari Mwalimu Chenge Marwa ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kufanya Uwekezaji mkubwa wa miundombinu katika shule hiyo, hali ambayo amesema imeendelea kuwafanya wanafunzi kufanya vizuri sana katika mitihani ya kuhitimu kidato cha sita.



More Stories
Rais Samia atoa msaada kwa kituo kinachohifadhi wasichana waliokimbia ukatili
Mo Dewji na Urithi anaoujenga ,unavyoenda mbali zaidi ya mafanikio binafsi
Mulika Community kusaidia Serikali kukomesha vitendo vya ukatili