May 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Tabora, Mashamu Paul Ruzoka. (Picha na TEC).

Miziki inayopigwa huko baa usiku inakwaza asema Askofu Ruzoka

Na Tiganya Vincent, Tabora

MHASHAMU Baba Askofu Mkuu, Paul Ruzoka wa Jimbo Kuu Katoliki Tabora amevitaka vyombo vinavyosimamia sheria za uendeshaji wa sehemu za starehe hasa kwenye baa kuhahakisha miziki inayopigwa katika biashara zao hauleti kero kwa watu wengine.

Hali hiyo inatokana na kuzuka kwa tabia ya baadhi ya wamiliki wa baa jirani na Chuo cha Utumishi wa Umma(UHAZILI) kufungulia muziki (disco) kwa sauti ya juu usiku kuchwa na kusababisha wakazi walio jirani kushindwa kulala.

Askofu Mkuu Ruzoka alitoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki wakati wa mahubiri.

“Katika maeneo hayo kuna watu wanahitaji utulivu ili waweze kusali, lakini wanashindwa kwa sababu miziki inafunguliwa inakera, kuna wagonjwa katika maeneo hayo wanahitaji utulivu lakini miziki inayopigwa inawaongezea maumivu…kuna watu wanataka kupumzika baada ya majukumu, lakini hawapati haki yao kwa sababu ya kelele,” alisema.

Alisema, upo uwezekano watu wanaosimamia utekelezaji wa sheria ni wateja wa maeneo hayo ndio maana wameshindwa kusimamia Sheria za Uendeshaji wa baa hizo ili kulinda za watu wengine.

Mhashamu Baba Askofu Mkuu Ruzoka aliongeza hata wanaokuwa katika maeneo hayo hawazingatii maelekezo ya wataalamu wa sekta ya afya ya kujikinga na ugonjwa wa Covid-19 wa kukaa umbali walau mita moja na nusu.

“Wakati viongozi mbalimbali za dini na Serikali na waumini wakizingatia ukaaji wakati wa ibada na wakisisitiza kuendelea kuomba kwenye maeneo hayo wao hawazingatii maelezo ya kitaalamu jambo ambalo ni baya,”alisema.

Mmoja wa wakazi wa Kanyeye Joseph Kulwa alisema, kuna tatizo kubwa la ufunguliaji wa miziki katika kata hiyo na limekuwa sugu.

Alisema, karibu baa kubwa zote zinapiga mziki hadi usiku wa manane bili kuwa na kumbi ambazo zinazuia sauti kutoka nje na kuwa kero kwa watu wengine ambao wamelala.