July 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa

Mikataba ya viwanda vya Sukari kupitiwa

Ikizingatiwa hakutakuwa na uhaba wa sukari, hivyo haitaagizwa kutoka nje, Waziri Bashungwa aanza ukaguzi

Na Mwandishi Wetu

WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa amewataka wenye viwanda vya sukari nchini kurejea mikataba ya uzalishaji walioafikiana na Serikali kujiridhisha iwapo inaenda sambamba na masharti waliokubaliana.

Bashungwa aliyasema hayo mkoani Kilimanjaro alipofanya ziara katika kiwanda cha kuzalisha sukari cha TPC ili kujiridhisha na hali ya uzalishaji viwandani hapa.

“Kuna viwanda vinne Kagera Sugar, Mtibwa Sugar, Kilombero Sugar na TPC wakati vinabinafsishwa vilipewa malengo ya kuongeza uzalishaji wake.

TPC kilipobinafsishwa mwaka 2007 kilipewa malengo ya kuzalisha tani 75,000, lakini kwa sasa kinazalisha tani 100,000 kwa mwaka,”alisema Waziri Bashungwa na kuongeza;

“Baada ya kutembelea TPC wanawatumia ujumbe viwanda vingine kama Kagera Sugar, Mtibwa Sugar, Kilombero Sugar kurejea mikataba ya ubinafsishaji ili kujiridhisha kama wanaenda sambamba na mikataba hiyo.”

Bashungwa aliongeza kuwa viwanda vya Kagera Sugar, Mtibwa Sugar na Kilombero kurejea mikataba ya uzalishaji kuna malengo ya Serikali, nitapita kuangalia kama mmezingatia mnafuatilia mikataba ya uzalishaji.

“Kama watakuwa wameshindwa kutimiza malengo hayo basi watakuwa wanatukwamisha. Rais John Magufuli alipoingia madarakani mwaka 2015, aliweka malengo ya kuwa nchi ya viwanda ili tujitegemee katika uzalishaji wa vitu kama sukari.” Alisema.

Bashungwa aliendelea kusema kuwa viwanda hivyo vinatoa ajira kubwa kwa kinamama na vijana, mfano hapa TPC peke yake wanatoa ajira 4,000 za moja kwa moja achilia mbali zile zinazokuja kutokana na uzalishaji na usafirishaji.

“Endapo viwanda vya kuzalisha sukari vya Kagera, Mtibwa na Kilombero vitazingatia mkataba wa uzalishaji basi hakutakuwa na uhaba wa sukari hapa nchini. Tutaachana na masuala ya kuagiza sukari kila mwaka pamoja na upungufu wa bidhaa hiyo,”alisema.

“Nia ya Serikali ni kuzalisha sukari kwa wingi ili kuuza ndani ya nchi na nje ya nchi katika masoko ya EAC, SADC,COMESA kwa kuwa nchi yetu ni mwanachama wa jumuiya hizo zote”.Alisisitiza Bashungwa.

Aidha aliwaonya wafanyabiashara wanaosambaza sukari nchini ambao wanatumia kipindi cha mfungo wa Ramadhani kuongeza bei ya Sukari, kuwa Serikali haitawafumbia macho kwa kufanya kitendo hicho.

Ole wenu tukiwabainisha tutawawafutia leseni za biashara ,hamtafanya biashara tena kama mkibainika kupandisha bei ya sukari.

Aliongeza kusema kuwa Serikali imetoa ukomo wa bei za sukari ya kiwango cha juu si lazima mtu akauza bei hiyo.