September 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mhariri Mkuu Clouds kuwania uongozi Jukwaa la Wahariri nchini

Na Iddy Lugendo, TimesMajira Online, Dar es Salaam

Joyce Shebe akijaza fomu za kugombea kuongoza TEF katika nafasi ya Makamu Mwenyekiti

MHARIRI Mkuu wa Clouds Media ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Utendaji ya Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Joyce Shebe amejitosa katika kinyang’anyiro cha kuwania nafasi ya Makamu Mwenyeki wa jukwaa hilo.

Shebe amejaza na kumkabidhi fomu kwa Mratibu wa Jukwaa hilo Prisca Kabendera leo katika ofisi za TEF Jijini Dar es Salaam.

Shebe ameeleza dhamira yake ya kuliongoza jukwaa ili kufikia malengo yake katika kipindi kijacho cha uongozi.

TEF ndio chombo kikubwa kabisa nchini kinachounganisha wahariri na wadau kutoka katika vyombo mbalimbali vya habari nchini na tasnia nzima ya habari.

TEF inatarajia kufanya Uchaguzi Mkuu mwaka huu ambapo itapata safu mpya ya uongozi itakayongoza kwa kipindi cha miaka 4.

Joyce Shebe(kushoto) akikabidhi fomu kwa Prisca Kabendera ambaye ni Mratibu wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) mapema leo katika ofisi za Jukwaa hilo. Anayeshuhudia ni Nevile Meena, Katibu wa Jukwaa la Wahariri Tanzania. Picha zote na Iddy Lugendo

Mratibu wa TEF, Prisca amesema mpaka sasa wajumbe wengi wameshachukua fomu ili kuwania nafasi za Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti pamoja na nafasi za wajumbe wa Kamati ya Utendaji.

“Mwamko ni mkubwa, mijadala pia ni mingi na wajumbe wamejitokeza na kuchukua fomu kuonesha nia ya kugombea nafasi mbalimbali za TEF.

“Uchaguzi huu ni muhimu kwa tasnia yetu ya habari, na tarehe ya mwisho ni saa kumi kamili jioni Mei 12 , mwaka huu, ambapo idadi kamili ya waliochukua fomu itajulikana.” amesema Prisca.