March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mgombea wa Urais kupitia CCM, Dkt. Samia awashukuru wananchi wa Uyui,Urambo na Kaliua

Na Mwandishi wetu ,Timesmajira

Mgombea wa Urais kupitia CCM, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewashukuru wananchi wa Uyui kwa mapokezi makubwa na kuwakumbusha ziara yake ya Mei 17,2022 ambapo alifungua barabara ya kilomita 85 ya Nyahua chanya. 

Amesema wakati huo wananchi walimueleza changamoto ya upungufu wa watumishi wa afya na elimu, na sasa serikali imewaletea watumishi wa afya 161 na walimu 412. 

Aidha, amewakumbusha kuwa ndani ya siku 100 za uongozi wake serikali itaweza kuajiri watumishi 5,000 katika sekta ya afya na 7,000 katika sekta ya elimu, na baadhi yao watapelekwa Uyui.

AFYA

Mgombea wa Urais kupitia CCM,Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema shilingi bilioni 8.2 zimetumika kuboresha hospitali ya wilaya, kujenga vituo vya afya vipya vitano, zahanati mpya 17 na kupeleka magari matatu ya wagonjwa.

Dkt. Samia amewaahidi wananchi wa Uyui kuwa endapo watamchagua yeye na wagombea wa CCM, itaendelea kusaidia kukamilisha vituo vya afya ambavyo wananchi wameanzisha, hususan katika maeneo ya Goweko na Usagari.

ELIMU

Kuhusu sekta elimu, Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema shule za sekondari zimeongezeka kutoka saba hadi 34 katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wake, huku idadi ya wanafunzi ikipanda kutoka 12,000 hadi 17,500.

 Ameongeza kuwa shule za msingi zimeongezeka kutoka 158 hadi 182, na serikali imeendeleza sera ya elimu bila ada, kujenga madarasa ya chekechea na kanzisha programu mpya za elimu ya awali.

Kukamilisha ujenzi wa chuo cha

VETA na kuweka viwanda vidogovidogo kwa ajili ya kuongeza thamani ya mazao ya vijana.

KILIMO

Akizungumzia kilimo na mifugo, Dkt. Samia amesema serikali imejenga skimu za umwagiliaji katika maeneo ya Goweko na Ulianyama, na imeendelea kutoa ruzuku za mbolea na mbegu pamoja na dawa za chanjo kwa wafugaji.

Amesema kuwa endapo itachaguliwa tena kuongoza na kuunda serikali katika uchaguzi mkuu wa Oktoba itaendelea kujenga majosho na mabwawa kwa ajili ya mifugo. 

Alizungumzia pia wakulima wa tumbaku wenye madai ya muda mrefu Dkt. Samia amewahidi kuwa serikali ipo kwenye mazungumzo na kampuni husika na wakulima watalipwa. 

Amesema serikali imeongeza makampuni ya kununua tumbaku ili kuleta ushindani.

MAJI

Kuhusu sekta ya maji, mgombea wa Urais Dkt. Samia amesema serikali yake

imekamilisha miradi 15 ya maji ambayo imeongeza upatikanaji wa huduma

kufikia asilimia 67, Dkt. Samia amewaahidi wananchi wa Uyui kuwa iwapo watamchagua atajenga tanki la maji lenye ujazo wa lita milioni moja kupitia mradi wa Ziwa Victoria katika kata ya Ilolangulu litakalohudumia pia kata za Kalola, Isila, Dono na Mabana. 

Ameongeza kuwa miradi mingine katika Kigwa,Kizengi na bwawa la Igombe ipo katika hatua nzuri na itakamilishwa.

MIUNDOMBINU

Kuhusu miundombinu, Dkt. Samia amewajulisha wananchi kuwa usanifu

wa Daraja la Mto Loya umekamilika, fedha zimetengwa na sasa serikali

inatafuta mkandarasi ili ujenzi uanze.

 Ameongeza kuwa serikali yake

itakapopewa ridhaa na watanzania hasa wa Uyui itaendelea kuboresha

barabara za vijiji ili ziweze kupitika wakati wote, ikiwemo barabara ya

Ilolangulu–Isenga–Kasisi A na barabara ya Ndono–Mfuluma–Makazi.

 Aidha,amesema ombi la barabara ya Tabora–Kahama limepokelewa na serikali

italifanyia kazi.

UMEME

Mgombea wa Urais kupitia CCM Dkt. Samia Suluhu Hassan amewaomba

wananchi wa Wilaya ya Uyui mkoani Tabora kukichagua chama cha

Mapinduzi (CCM) katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi oktoba mwaka huu ili serikali yake iweze kufikisha umeme katika vitongoji vyote vilivyosalia kwenye wilaya ya Uyui katika kipindi cha mwaka 2025-2030, kwani kwa miaka mine ya uongozi wake 2021-2025 ameweza kufikisha umeme katika vijiji vyote na sasa kazi iliyobaki ni vitongoji.

URAMBO- TABORA

Mgombea wa Urais kupitia CCM, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan,

ameendelea na mikutano ya kampeni katika mkoa wa Tabora ambapo

amefanya mkutano mkubwa wa hadhara akiwa Urambo ambapo

amewahakikishia wananchi wa Urambo kuwa chama cha Mapinduzi (CCM)

kikipewa ridhaa na watanzania hasa wa jimbo la Urambo kitaendelea

kutekeleza ahadi zake kwa vitendo.

 Dkt. Samia amesema chama

kimetekeleza asilimia 90 ya ilani ya uchaguzi wa 2020-2025 na kipo katika

hatua za kukamilisha machache yaliosalia. 

KILIMO/ ZAO LA TUMBAKU

Akizungumza kuhusu zao la tumbaku ambalo ni uti wa mgongo wa uchumi wa

Urambo, Mhe. Dkt. Samia amesema uzalishaji umeongezeka kutoka tani

11,208 mwaka 2021/2022 hadi tani 20,492 mwaka 2025. 

Ameongeza kuwa

thamani ya mauzo imepanda kutoka dola milioni 11 mwaka 2021/2022 hadi

dola milioni 50 mwaka 2024/2025, huku bei ya tumbaku pia ikiongezeka kutoka

dola moja kwa kilo hadi dola 2.5 kwa kilo.

 Amesema awali tumbaku ilinunuliwa

kwa kuchaguliwa lakini sasa serikali imehakikisha kuwa makampuni

yananunua yote, na kiwanda cha kuongeza thamani kipo Morogoro kabla ya

kusafirishwa nje ya nchi.

Katia hatua nyingine  Rais Samia ambaye pia ni mgombea wa Urais

kupitia CCM amewaasa wakulima kupunguza ukataji miti na kutumia teknolojia mpya ya kukausha tumbaku ili kulinda mazingira, kuongeza mvua na kuhifadhi

vyanzo vya maji. 

Pia ameeleza kuwa serikali yake imeimarisha sekta ya kilimo

kwa kujenga skimu mbili za umwagiliaji katika maeneo ya Uyogo na Izimbili, na

kuanzisha soko la mazao.

ELIMU

Kuhusu elimu, Dkt. Samia ameomba wananchi wa Urambo kumchagua

yeye sambamba na wagombea wengine wa CCM ili kufanikisha ujenzi wa

shule 12 mpya za msingi na sekondari sambamba na kuendeleza na

kuboresha miundombinu ya Elimu katika jimbo la Urambo.

MIUNDOMBINU

Akizungumzia miundombinu ya barabara, Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye

ni mgombea wa Urais wa kwanza mwanamke ndani CCM, amewaambia

wananchi wa Urambo kuwa serikali yake imejenga barabara mbalimbali kwa

kiwango cha lami katika maeneo ya Emirates–Mnyonge–Usoke, Urambo–

Ukwanga, Igunguri–Milambo, Urambo–Itebulanda–Kangeme, Izimbili–

Mabama, Tebela–Uwima, Usoke–Kalembela na Kindwa. Amewaomba

wananchi wa Urambo kumchagua ili aendelee kujenga barabara za Urambo

kwa kiwango cha lami katika maeneo yote muhimu.

Aidha, Dkt. Samia amewaahidi wananchi wa Urambo serikali yake ikipata

ridhaa itajenga soko jipya katika mtaa wa St. Vicent na kuendeleza ujenzi wa

vibanda vya biashara katika stendi kuu ya mabasi. Aliongeza kuwa huduma

za afya, umeme na maji bado zitaendelea kupewa kipaumbele na serikali

itaendelea kuzitekeleza kulingana na mahitaji ya wananchi.

KALIUA- TABORA

Mgombea wa Urais kupitia CCM, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewashukuru

wananchi wa Kaliua kwa kujitokeza kwa wingi na kueleza kuwa serikali tayari

imetekeleza mambo mengi katika maji, umeme, barabara, afya na elimu.

AFYA

Dkt. Samia amesema sekta ya afya ni muhimu kwa ustawi wa wananchi na

kwamba serikali yake ikipewa ridhaa na watanzania itaendeleza ujenzi wa

vituo vya afya katika maeneo ya Ukumbi, Siganga, Kashishi, Ugunga na

Ichemba, na kukamilisha zahanati nane katika maeneo ya Imalaupina,

Ushokola, Igombe, Sitini, Mnange, Keza, Ikonongo, Igwisi na Mwahajala,

zikiwemo na nyumba za watumishi. Aidha, alisema serikali yake ikipewa ridhaa

na wananchi itakamilisha ujenzi wa hospitali ya wilaya ya Kaliua ikiwemo jengo

la mama na mtoto.

MIUNDOMBINU

Kuhusu miundombinu ya barabara,  Dkt. Samia amesema endapo

atachaguliwa atafanikisha ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami katika

maeneo ya Banyanga, Masudi–Silimu–Msufini, Kisamvu, Machibya 1, Kibonde,

Ostabei na KKKT. Pia alisema barabara za changarawe zitajengwa katika

maeneo ya King’wang’okoko – Usonga, Taba – Imara–Keza, Ichemba –

Mwande, Sasu – King’wang’koko – Seleli, Mpanda–Mlowoka – Mwahajala,

Uyowa – Msungwa – Uliyankulu, Ufukutwa Tuombemungu–Mkuyuni na Keza –

Igombe. 

Ameongeza kuwa barabara mpya zitafunguliwa katika maeneo ya

Seleli, Mwahajala na Uliyankulu. Pia aliongeza kuwa ombi la barabara ya

Kahama–Tabora limepokelewa na litafanyiwa kazi.

MAJI

Mgombea wa Urais kupitia chama cha Mapinduzi ( CCM) Dkt. Samia Suluhu

Hassan amewaomba wananchi wa jimbo la Kaliua mkoani Tabora

kumchagua tena katika nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

ili aweze kufanikisha ujenzi wa chujio la maji kwenye vijiji 17 ili kuhakikisha

wananchi wanapata maji safi na salama, pamoja na bwawa jipya la

Zugimlole na miradi mingine ya maji. 

Aidha, amesema uchimbaji wa visima

utaendelea kwa lengo la kumaliza kabisa changamoto ya maji ndani ya

miaka mitano.

MIFUGO

Kuhusu sekta ya mifugo, Dkt. Samia serikali ya CCM ambayo yeye ni

mgombea wake ikichaguliwa itaanzisha ranchi na shamba la malisho na uhamilishaji, kujenga minada na machinjio ya kisasa katika eneo la Kasungu,

pamoja na majosho ya mifugo katika maeneo ya Makingi na Mitimitano.

UPIMAJI WA VIWANJA

Katika hatua nyingine Dkt. Samia amesema serikali yake itahamasisha upimaji

na umilikishaji wa viwanja katika maeneo ya Kasungu, Ufukutwa na Ushokola

ili wananchi wapate maeneo ya biashara na makazi.