May 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mgao wa Umeme Wilaya ya Temeke kumalizika Machi 2024-RC Chalamila

Na Heri Shaaban , TimesMajira Online, Temeke

MKUU wa Mkoa Dar es Salaam Albert John Chalamila amesema katika wilaya ya Temeke changamoto ya kukatika kwa umeme itapungua mwezi machi mwaka huu mara baada kumalizika kwa Uboreshaji na Uwekezaji wa Miundombinu ya Umeme, kwenye kituo Kupozea na kusafirisha umeme kwenye Mradi wa Kurasini-Mbagala.

Mkuu wa Mkoa Albert Chalamila alisema hayo wakati wa ziara yake ndani ya jimbo la Temeke iliyolenga kuangalia miradi ya maendeleo ikiwemo miundombinu ya Barabara na kuzungumza na Wananchi kupitia mikutano ya hadhara ili kusikiliza na kutatua kero zao.

“Nitazungumza na watu wanaokwamisha mradi huu ili uweze kufanikiwa napongeza Serikali yetu ya Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuwekeza kwenye sekta ya Nishati ya umeme ikiwemo Bwawa la Mwalimu Julius Nyerere “alisema Chalamila.

Kwa upande wake Meneja wa TANESCO Mkoa wa Temeke Mhandisi Ezekiel Mashola alisema kwa sasa hali ya Upatikanaji wa umeme katika eneo la Kurasini na Mbagala sio ya Kuridhisha ndio, Nishati hiyo imekuwa ikitolewa kwa Mgao ili wananchi waweze kupata umeme wa kutosha, ambapo Serikali kwa kuliona hilo imekuja na miradi mikubwa miwili kutoka kituo cha kupoza umeme ILALA kwenda Kurasini baadae watatoa Kurasini ili kupeleka eneo la Dege.

Mhandisi Mashola alisema kukamilika kwa mradi huo kutaenda kutatua changamoto ya umeme kukatika mara kwa mara kwenye maeneo ya Mbagala, Kurasini na Temeke, huku akibainisha mradi huo umegharimu shilingi bilioni 31 utamalizika Machi.

Mbunge wa Jimbo la Temeke Dorothy Kilave alitumia fursa hiyo kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayofanya ya utekelezaji wa Ilani ya chama cha Mapinduzi CCM na miradi mikubwa ya maendeleo.

Mbunge Dorothy Kilave aliwataka wananchi wa jimbo la Temeke kuunga mkono juhudi za Serikali ya awamu ya sita ya Rais wa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo amefanya mambo makubwa sekta ya Elimu, Afya ,na miundombinu ya Barabara..

Ziara ya mkuu wa mkoa Albert Chalamila katika Jimbo la Temeke alitembelea mradi wa ujenzi wa waya wa ardhini msongo wa Kilovolti 132 kutoka Ilala kwenda Kurasini ,kutembelea ujenzi wa shule ya mazoezi ya sekondari Changombe yenye vyumba vya madarasa saba na matundu kumi ya vyoo ujenzi wa barabara ya zege Miburani,na vyumba 16 vya madarasa 16 na matundu na matundu 25 ya vyoo jengo la Utawala shule ya Msingi Ushirika yombo vituka .