May 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

MCB yazindua kapu la ‘Mwalimusanta’

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online

KATIKA kuelekea msimu wa sikukuu za mwisho wa mwaka, Benki ya Biashara ya Mwalimu (MCB) imezindua kampeni ya kapu la Mwalimusanta yenye lengo la kutoa zawadi kwa wateja wake wakiwemo wastaafu.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam Desemba 6 2023, Anna Mbajo kutoka Idara ya Masoko ya Benki hiyo amesema kampeni hiyo imelenga kurudisha shukrani kwa wateja wake katika kipindi chote cha mwaka walichofanya wote biashara.

Amesema kwa mwaka huu kapu la Mwalimusata litatoa zawadi kwa makundi mawili ambayo ni wateja wa kawaida na wastaafu watarajiwa na wale ambao tayari wamestaafu.

Mbajo amesema kupitia akaunti ya muda maalumu pindi Mstaafu atakapowekeza katika benki hiyo kiasi cha milioni 10 na kuendelea atapata faida ya uwekezaji huo kwa asilimia 12 kwa mwaka na kuendelea.

“Mstaafu atapata faida hii ya asilimia 12 kwa kila mwaka ambapo ataweza kuichukua wakati wowote anapohitaji au pale mwanzoni anapofika baada ya kuweka fedha zake na baadae kupigiwa mahesabu yake ,”amesema.

Ameongeza kuwa Mstaafu huyo atapata faida na kuichukua kwa kila mwezi, miezi mitatu baada ya miezi sita… uwekezaji huu unaanzia miaka 2 na asilimia atakayopatiwa ni 12 hii ni faida mojawapo.

Pia ameongeza kuwa kutokana na kuwepo kwa majanga mbalimbali benki hiyo imeona katika kila uwekezaji atakaoufanya Mstaafu atakatiwa bima ya nyumba bure kwa yule anayemiliki na kwa ambaye ana nyumba atakatiwa bima ya thamani bure.

“Mbali na kufanya uwekezaji katika akaunti ya muda maalumu pia mstaafu ataweza kukopa kwa asilimia 80 ya kile alichokiwekeza ….lakini zaidi ya kukopa kupitia akaunti yake pia anaweza kukopa katika mikopo yetu mingine ikiwemo ule wa mlinde mstaafu,”amesema.

Aidha ametoa wito kwa wastaafu wote kuchangamkia uwekezaji huo ambao ni salama na uhakika utakaomuwezesha kupata faida.

Kwa upande wake Elilumba Kinyau kutoka Idara ya Huduma za Kidigitali za kibenki amesema katika kutambua kuwa dunia inaendeshwa kidigitali benki hiyo imeona ni vyema kutoa zawadi kwa wateja wao ambao watafanya muamala kupitia kwa wakala bila ya kutumia kadi.

Amesema mteja anachotakiwa ni kufanya miamala kupitia kiwango chochote ataweza kupata nafasi ya kujishindia kiasi cha 50,000.

“Zawadi hii itatolewa kwa mteja yoyote atakayefanya muamala kwa wingi bila kadi kupitia kwa wakala, kila wiki wateja watano wataweza kujishindia zawadi hii,”amesema.