October 1, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mbeya waainisha vituo 210 uchaguzi serikali za mitaa

Na Esther Macha, Timesmajira Online, Mbeya

JUMLA ya vituo 210 vya kupigia kura kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika Novemba 27, mwaka huu vimeanishwa katika mitaa mbalimbali ya Halmashauri ya jiji la Mbeya.

Akitoa taarifa kwa waandishi wa habari  Septemba 30, mwaka huu wakati wa mafunzo kwa wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi katika Halmashauri ya jiji Mbeya,Mchumi jijini hapo,Ally Nnunduma amesema hadi Sasa vituo 210 vitakavyotumika kwenye zoezi la uchaguzi wa serikali za mitaa vimeanishwa.

Ally amesema Kuna uwezekano vituo vingine vikaongezwa siku za usoni kulingana na mahitaji pamoja na Mazingira ya wakati huo, lakini kwa Sasa vituo vilioanishwa kwa ajili ya kujiandikishia na kupiga kura ni 210.

“Jiji la Mbeya tunazo tarafa mbili,kwa maana Iyunga na Sisimba, tunazo kata 36 na mitaa 181,Sasa kwenye hiyo mitaa ndio uchaguzi unaenda kufanyika huko” amesema

Amesema wahusika ambao watashiriki kupiga kura ni lazima wawe na umri wa kuanzia miaka 18 na kuendelea na lazima wawe wamejiandisha sehemu husika,lakini kwa upande wa wagombea wanapaswa kuwa chini ya udhamini wa vyama vyao vya siasa na wawe na umri wa kuanzia miaka 21.

Akitoa maelekezo kwa wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi kwenye kata,msimamizi Msaidizi Halmashauri ya jiji la Mbeya Davis Mbembela amewataka kufuata taratibuz Sheria na miongozo ya uchaguzi wa serikali za mitaa.

Pia katika mafunzo hayo wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi walikula kiapo cha uaminifu mbele ya hakimu mkazi Teddy Mlimba.