September 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mazungumzo ya Rais Samia, Xi Jinping na alama ya uhusiano uliodumu kwa miaka 60

Na Mwandishi Wetu,Timesmajiraonline

ZIARA ya Rais Samia Suluhu Hassan nchini Chini aliyoianza jana nchini imeendelea kufuatiliwa kwa karibu na wananchi wa mataifa hayo wawili, achia bara zima la Afrika, ambalo linafuatilia kwa karibu Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC).

Juzi Rais Samia , alifanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Watu wa China, Xi Jinping yaliyofanyika katika ukumbi wa The Great Hall of the People unathibitisha kupanda kwa uhusiano wa kirafiki kati ya Tanzania na China.

Ikumbukwe kwamba wakati anaondoka nchini tayari Rais Samia alikuwa ameelezea imani yake kuwa mkutano wa FOCAC utakuwa na mchango mpya katika kuimarisha ushirikiano wa kirafiki kati ya Afrika na China na kuhamasisha mchakato wa viwanda na kilimo cha kisasa barani Afrika.

Kabla ya mkutano huo, juzi viongozi wao ( Rais Samia na Xi Jinping) walikuwa mazungumzo ambayo yalilenga kuimarisha uhusiano baina ya mataifa hayo mawili.

Kikubwa zaidi ni kauli iliyotolewa na Rais Xi Jinping kwamba China iko tayari kuimarisha ushirikiano wa kimkakati kati yake na Tanzania ili kuleta manufaa zaidi kwa nchi zote mbili na kuendeleza uhusiano wa kihistoria ulioasisia na waasisi na kurithiwa na vizazi vya sasa.

Kauli hiyo ya Rais Xi Jinping ni uthibitisho tosa kwamba China ni rafiki mzuri zaidi wa Tanzania, uhusiano huo unatoa mchango muhimu kwa Tanzania katika nyanja mbalimbali za kiuchumi hivyo ziara hiyo ya Rais Samia nchini China inatoa fursa nyingi kwa maendeleo ya uhusiano kati ya Tanzania na China, na kupanua zaidi ushirikiano wa kibiashara kati ya nchi hizo mbili.

Wajumbe wa mkutano wa Rais wa China, Xi Jinping na Rais Samia Suluhu Hassan, wakifuatilia mazungumzo ya viongozi hao yalyofanyika juzi katika ukumbi wa The Great Hall of the People, nchini China

Hiyo inathibitishwa na kauli ya Rais Samia aliyoitoa juzi wakati akizungumza na Rais Xi Jinping,ambapo pamoja na mambo mengine alitoa wito kwa sekta binafsi nchini China kuwekeza Tanzania katika uzalishaji wa vyanzo vya nishati mbadala na miundombinu ya usambazaji.

“Uhusiano wa nchi hizi mbili ni muhimu na ninatoa wito wa kuendelea kudumisha ushirikiano katika nyanja mbalimbali pamoja na kuendeleza ushirikiano katika maeneo ya kuendeleza miundombinu na kukuza uwekezaji (Belt and Road Initiative) ili kuleta manufaa yanayoonekana kwa wananchi,” anasema Rais Samia kwenye mazungumzo na Rais Xi Jinping ambaye ni miongoni mwa viongozi wa mataifa makubwa duniani.

Katika kuthibitisha uaminifu wake kwaTanzania, Rais Xi Jinping anasema; .” China inaiona Tanzania kuwa ni mfano mzuri wa mahusiano kati ya nchi zinazoendelea katika muktadha wa ushirikiano wa China na nchi za Afrika.”

Uhusiano wa China na Tanzania ambao umeendelea kuimarishwa na viongozi wa mataifa hayo mawawili kama ilivyokuwa kwa watangulizi wao, ndio umezidi kuwasukuma waendelee kukubaliana kuendelea kubadilishana uzoefu na kupeana mafunzo katika maeneo mbalimbali ya kiserikali kwa manufaa ya wananchi wa nchi hizo.

Kwa mantiki hiyo ziara hiyo ya Rais Samia nchini China itafungua ukurasa mpya wa uhusiano kati ya China na Tanzania.

Kwa mantiki huyo pande hizo mbili China na Tanzania zinapaswa kutilia maanani umuhimu wa kimkakati, kimsingi na kiuongozi wa ushirikiano na kuitumia vizuri fursa ya ziara ya Rais Samia nchini China.

Baadhi ya wajumbe wa Rais wa China Xi Jinping wakifuatilia mazungumzo baina ya Rais wa nchi hiyo na Rais Samia Suluhu Hassan yaliyofanyika juzi kwenye ukumbi wa The Great Hall of the People.

Pia, pande hizo mbili zinatakiwa kutilia maanani ushirikiano wa aina mpya kati ya nchi hizi mbili katika sekta za uchumi na biashara, uwekezaji, ujenzi wa miundombinu ya mawasiliano pamoja na shughuli za utalii, kilimo, mradi wa TEHAMA, na uchumi wa kidijita.

Lakini pia, pande hizo mbili zinatakiwa kutilia maanani zaidi jinsi yakuongeza zaidi maelewano kati ya watu wa mataifa hayo, kuimarisa mawasiliano katika utamaduni, hasa mawasiliano kati ya vijana wa China na Tanzania.

Hiyo ni kwa sababu ushirikiano kati ya China na Tanzania siyo tu unanufaisha watu wa China na Tanzania, bali pia unatoa mchango kwa kujenga Afrika nzuri yenye amani na masikilizano zaidi.

Reli ya TAZARA ndiyo alama ya ushirikiano kati ya China na Afrika. Kwa kuthibitisha hilo, baada ya mazungumzo Rais Samia, Rais Xi Jinping, baadaye walifanya mazungumzo yaliyomshirikisha na Rais wa Zambia Hakainde Hichilema.

Rais Samia Suluhu Hassan akisalimia na mwenyeji wake, Rais wa China Xi Jinping, kabla ya kuanza kwa mkutano wao uliofanyika kwenye kumbi wa The Great Hall of the People.

Viongozi hao walishuhudia uwekaji saini wa Hati ya Makubaliano (MOU) baina ya Tanzania, Zambia na China kuhusu uboreshaji wa reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA)

Pia, akiwa kwenye ziara yake Rais Samia anawasilisha miradi minne kwa Serikali ya China kwa lengo la kupatiwa fedha za mkopo nafuu na msaada ya utekelezaji wake. Anatarajia kuiwasilisha katika mkutano wa kilele wa wakuu wa nchi na Serikali wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC), ambalo kwa miongo zaidi ya miwili sasa limekuwa likitumiwa na wakuu wa nchi za Afrika kwa madhumuni yanayofanana na hayo.

Miradi minne itakayowasilishwa na Rais Samia kwenye mkutano huo ni ujenzi wa mtandao wa mawasiliano vijijini awamu ya pili, ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa kilovoti 400 awamu ya pili na ya tatu, ujenzi wa vyuo vya ufundi stadi (Veta) awamu ya pili na ujenzi wa barabara za Zanzibar zenye urefu wa kilomita 277.

Taarifa h iliyotolewa Agosti 31, 2024 na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo alipozungumza na waandishi wa habari, jijini Dar es Salaam kuhusu ziara ya Rais Samia China alisema;

“Tanzania inatarajia kuwasilisha miradi mbalimbali ikiwemo mipya na ile ambayo haikuweza kutelezwa kwenye mpango uliopita wa FOCAC kwa sababu mbalimbali, ili iweze kupatiwa fedha za mkopo nafuu na msaada na kutekelezwa chini ya mpango kazi wa FOCAC mwaka 2025-2027.”

Balozi Kombo ametaja malengo matatu ya Tanzania kushiriki mkutano huo kuwa moja, kuendelea kudumisha ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na China ambao mwaka huu umetimiza miaka 60.

Pili ni kujadiliana na kukubaliana na Serikali ya China namna ya kuendelea kuongeza ushirikiano katika maeneo ya kipaumbele kama sekta ya miundombinu, mifumo ya chakula, biashara na uwekezaji, kubadilishana ujuzi, upatikanaji wa nishati safi na salama na kusaidia ujenzi wa uchumi wa kidijitali

Mambo hayo tayari yamewekwa wazi kupitia mazungumzo ya Rais Samia na Xi Jinping yaliyofanyika juzi katika ukumbi wa The Great Hall of the People

Pia Balozi Kombo anasema ziara hiyo itaibua fursa mpya za ushirikiano kwa manufaa ya pande zote mbili, kutangaza maboresho makubwa yaliyofanywa na Serikali katika sheria za sekta ya biashara na uwekezaji ili kuvutia wawekezaji wengi zaidi.

Juzi Rais Samia amekamilika ratiba mbili za ziara zake ambapo ratiba zingine ziliendelea jana. Kwa juzi akiwa China, Rais Samia amefanya mkutano na Rais Xi Jinping kama tupoona hapo mbili na kujadili masuala mbalimbali ya ushirikiano kati ya mataifa hayo mawili.

“Aidha, baada ya mazungumzo hayo walishiriki hafla ya kutia saini hati za makubaliano kuhusu kuifufua Reli ya TAZARA. Ratiba nyingi ya ziara ya Rais Samia ni kufanya mazungumzo na kampuni za China ambazo zipo tayari kufanya uwekezaji mkubwa na kufungua ofisi zao nchini Tanzania.

“Atakutana na kampuni kubwa za China kwa pamoja katika hafla ya chakula cha jioni, yenye lengo la kuhamasisha kufanya uwekezaji nchini Tanzania,” amesema.

Kwa mujibu wa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo uwekezaji wa China nchini umefikia Sh30 trilioni. Aidha Tangu kuanza kwake mwaka 2000 FOCAC imewezesha miradi mikubwa ya miundombinu barani Afrika, kama vile ujenzi wa barabara, reli, viwanja vya ndege, bandari pamoja na uwekezaji katika nishati.

Ushirikiano chini ya FOCAC umeongeza biashara kati ya Afrika na China huku nchi za Afrika zikipata soko kubwa kwa bidhaa zao za kilimo, madini na malighafi nyingine, na kunufaika na uagizaji wa bidhaa za bei nafuu kutoka China.