Fresha Kinasa,TimesMajiraOnline,Mara.
MAJADILIANO yenye Mapendekezo ya Uboreshaji wa ufundishaji, Ujifunzaji na Uelewa wa Wanafunzi katika Jimbo la Musoma Vijijini Mkoa wa Mara yanatarajia kufanyika Machi 25, 2025 hadi Machi 27, 2025.
Huku yakitarajiwa kuja na Mapendekezo kabambe ya kuimarisha ufanisi wa Sekta ya Elimu Jimboni humo.
Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini Prof. Sospter Muhongo,amefadhili na kuandaa Majadiliano hayo yatakayoangazia Sekta ya Elimu Musoma Vijijini kwa upana wake ambapo yatahudhuriwa na wataalamu akiwemo Dkt.Zabron Kengera kutoka UDSM,Dkt. George Kahangwa UDSM na Japhet Makongo Ubunifu Associates.
Kwa mujibu wa Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini Machi 19, 2025, imesema kuwa, Majadiliano hayo yatafanyika Ukumbi wa Kanisa Katoliki, Mugango kuanzia Machi 25, 2025, hadi Machi 27, 2025.
“Tarehe 25 March 2025, Asubuhi Saa 3-6 Walimu Taaluma Shule za Msingi & Sekondari. Mchana Saa 8- 11 jioni Viongozi Watendaji Kata (WEO Afisa Elimu Kata. Na Machi 26, 2025,
Asubuhi: Saa 3-6: Shule za Msingi Headteachers/Headmistresses. Mchana Saa 8- 11: Shule za Sekondari Headmasters/Headmistresses.”imeeleza sehemu ya Taarifa hiyo na kuongeza.
“Tarehe 27 Machi 2025 , Asubuhi Saa 3 -6 Mapendekezo kuwasilishwa
DC, DED, DEOs, Madiwani
Mbunge wa Jimbo. Mchana: Saa 8- 11 (Majumuhisho) Mgeni Rasmi Mkuu wa Wilaya ya Musoma Juma Chikoka atatoa maelekezo ya utekelezaji wa Mapendekezo.”
Aidha, Motisha zitatolewa siku ya kuhitimisha majadiliano hayo Machi 27, 2025, kwa waliofanya vizuri mwaka 2024, Wahusika ni Waalikwa wakiwemo Viongozi wa shule zote, Afisa Elimu Kata,Watendaji wa Vijiji (VEO),Watendaji wa Kata (WEO),Viongozi wa Halmashauri,Madiwani na Mbunge wa Jimbo hilo.
Kwa upande wao Wananchi wa Jimbo la Musoma Vijijini wakizungumza na Majira Online wamesema katika majadiliano hayo , wanaamini yatakuja na mikakati mbalimbali ikiwemo ya kuongeza ufaulu wa Wanafunzi kwa Masomo ya Sayansi na mbinu bora za ufundishaji wa masomo hayo.
“Namshukuru Prof. Muhongo kuandaa Jambo hili bora kabisa kwa ajili ya Sekta ya Elimu Jimboni mwetu, amegusa wadau wote, Jambo zuri Madiwani ambao ni Wawakilishi wa Wananchi watahudhuria Majadiliano hayo, changamoto za Wananchi naomba waziweke wazi zipatiwe ufumbuzi lipo suala la chakula shuleni baadhi ya Wazazi kuchangia ni wazito likiwekewa mikakati madhubuti litasaidia ufaulu kwa Watoto wetu.” amesema John Masatu Mkazi wa Kijiji cha Bukumi.
“Mbunge wetu anafanya kazi kubwa na nzuri ya kushirikiana na Wananchi kujenga maabara, anapiga harambee kwa juhudi zote na wakati mwingine anatumia pesa zake binafsi kulipa Walimu wa Muda wanaofundisha Masomo ya Sayansi katika shule Mbalimbali jimboni mwetu. Itapendeza pia kuona serikali inaleta Walimu wa Sayansi waje wasaidie kufundisha watoto wetu masomo hayo ambayo wigo wake ni mpana katika Soko la ajira na kujiajiri pia.”amesema Meshack Juma Mkazi wa Kijiji Etaro.
More Stories
Kamati ya kudumu ya Bunge yapongeza ujenzi wa jengo la Wizara ya Nishati Mtumba
Gawio kutoka kampuni ambazo Serikali ina hisa chache zapaa kwa asilimia 236
Pinda:Vijana tumieni fursa kupata maarifa ya ufundi stadi