October 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Magu yatakiwa kutenga fedha kujenga miundombinu ya maji

Na Daud Magesa, Timesmajira Online, Magu

KAMATI ya Siasa Mkoa wa Mwanza imeiagiza Halmashauri ya Wilaya ya Magu, kutenga fedha za mapato ya ndani zitumike kujenga miundombinu ya kuvuna maji na kuchimba visima katika taasisi za umma ili kukabiliana na changamoto ya maji.


Agizo hilo limetolewa leo na Mjumbe wa Kamati hiyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Mwanza, Mohamed Lukonge, baada ya kukagua ujenzi wa shule mpya ya msingi Igekemaja, wilayani Magu mkoani hapa .

“Kamati imekuja kukagua miradi ya maendeleo iliyotekelezwa na serikali ya hapa Igudija imetuletea zaidi ya milioni 500 kujenga shule mpya,”amesema.

Amesema Watanzania wana tatizo la kutovuna maji ya mvua, zikiwemo taasisi za umma,wanasubiri hadi waunganishwe na huduma ya maji ya bomba kwa gharama.


“Rai yangu kwa Halmashauri ya Magu tengeni fedha za mapato ya ndani kujenga miundombinu ya kuvuna maji ya mvua na chimbeni visima, tusisubiri kuletewa maji ,tumieni majengo haya kuvuna maji kwa matumizi ya watoto shuleni,”amesema Lukonge na kuongeza maji ya bomba yatakuja lakini yawe ni ziada.


Pia uongozi wa shule hiyo ya Igudija katika Kata ya Kisesa iliyojengwa hivi karibuni, kuitunza miundombinu hiyo itumike muda mrefu na kwa vizazi vijavyo,inaonesha uchakavu sababu ya utunzaji wa miundombinu hiyo usio imara.

Awali Mwalimu Mkuu wa shule hiyo Benfaxad Chiguru amesema shule hiyo imejengwa kwa kiasi cha milioni 504 za mradi wa BOOST ili kupunguza msongamano wa wanafunzi katika shule za pembezoni.

Kamati ya Siasa ya Mkoa wa Mwanza,ikiwa katika shule ya Sekondari Igekemaja, kukagua maabara mbili za masomo ya Kemia na Fizikia imesema serikali ina dhamira ya dhati ya kuboresha sekta ya elimu kwa kujenga miundombinu ya madarasa watoto wasome katika mazingira rafiki na kutoa elimu bure.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mwanza,Michael Masanja ‘Smart’ amesema Rais Dk. Samia anatambua umuhimu wa elimu kuwa ndio kila kitu,anafanya kazi kubwa ya kuwezesha watoto wapate elimu katika mazingira, hivyo awakataka wanafunzi wa shule hiyo kusoma kwa biidi ili watimize ndoto zao.

Aidha amewapongeza wananchi wa Igekemja kwa kujitoa kuchangia kiasi cha milioni 11.8 za ujenzi wa maabara za masomo ya sayansi (Kemia na Fizikia),hivyo wakamilishe madarasa yaliyopo watoto wasome katika mazingira bora ya kujifunzaia.

Pia,wazazi na walezi waone umuhimu kupeleka watoto kusoma katik shule hiyo, kwani bila wanafunzi na walimu miundombinu hiyo haitakuwa na maana.

Awali Baraka Mbassa amesema maabara hizo zimejengwa kwa ufadhili wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kwa sh. milioni 103.5 ili kuwezesha wanafunzi kujifunza masomo ya sayansi kwa vitendona kuongea ujuzi na kufanya utafiti wa kisayansi.

Katika mradi huo wa maabara mbili wananchi walichangia nguvu zao sawa na sh. milioni 11.8 huku TASAF ikitoa sh. milioni 92.4.