September 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Machifu,viongozi wa dini,watakiwa kuwakumbusha wazazi wajibu wao

Na Esther Macha, Timesmajira Online,Mbeya

SERIKALI mkoani Mbeya imewaomba viongozi wa Dini na Machifu, kutumia mikusanyiko ya watu kuwakumbusha wazazi na walezi, kuzungumza na watoto wao pamoja na kuwakagua,ili waweze kubaini kama wamefanyiwa vitendo vya ukatili.

Kauli hiyo imetolewa,Septemba 25,2024, na Mkuu wa Wilaya ya Mbeya , Beno Malisa,kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Juma Homera, katika ufunguzi wa kampeni ya “Tuwaambie kabla hawajaharibiwa”.Kampeni hiyo iliowalenga wanafunzi wa shule za msingi ,sekondari na vyuo.

“Watoto tukatoe ushirikiano kwa wazazi,lakini wazazi mkatimize wajibu wenu wa msingi.Tufuate misingi na taratibu zetu,za kuwalea watoto tunaowaleta duniani,”amesema Mkuu huyo wa Wilaya .

Amesema lengo la kampeni hiyo, ni kuwatahadharisha vijana na watoto,changamoto ambazo zinawakabiri pamoja na mazingira wanayokulia.Hivyo jamii itumie kampeni hiyo, kupeleka elimu kila kona,hali itanakayo saidia kuondoa mmonyoko wa maadili katika jamii .

“Mmomonyoko wa maadili, upo kwa watoto,ambao hawajajitambua kwa asimilia 100, na kuhitaji usaidizi wa walezi ,walimu na jamii kwa ujumla ili wawe watoto salama wa Taifa la leo pamoja na kesho,”

Amesema Mkoa wa Mbeya wamejidhatiti,kuhakikisha elimu ya ukatili wa kijinsia inafika kila mahali.Pia atakaye kuwa kinyume na kampeni hiyo na kuendeleza tamaduni zisizo sawa kwa watoto,kwa kuwafanyia ukatili ,sheria zipo wazi.

“Mkoa wa Mbeya umedhamiria kuunga jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan,za kuhakikisha watoto,wanakua kiakili, kimaadili na kimwili.Hivyo Jeshi la Polisi lipo imara, kwa kushirikiana na Dawati la Jinsia,tufanya kampeni hii kukumbushana wajibu wetu,“amesema Malisa.

Kwa Upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya ,Benjamin Kuzaga,amesema kampeni hiyo ya “Tuwaambie kabla hawajaharibiwa”, kitaifa ilizinduliwa Mkoa wa Njombe,Agosti 29,2024,na Mkoa wa Mbeya imezinduliwa leo ambapo kwa Wilaya zote walishazindua kampeni hiyo.

Kuzaga amesema, lengo la kampeni hiyo, imeanzishwa kwa ajili ya kusaidiana na wazazi ,walimu na walezi ili kuweza kuwalinda watoto, na kupata taarifa za watu ambao wanahusika na vitendo vya kubaka ,vipigo ambavyo vinawaathiri watoto.

Mkuu wa Dawati la Jinsia Mkoa wa Mbeya, ASP, Veroca Ponela,amesema kupitia kampeni hiyo,elimu itaendelea kutolewa kwenye shule za msingi ,sekondari ,vyuo vya kati na vyuo vya elimu ya juu, lengo ni kupinga ukatili unaoendelea katika jamii,ili watoto waweze kutoa taarifa pindi watakapofanyia vitendo hivyo.

Ofisa Ustawi wa Jamii kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya,Salum Mayendi, amesema kuwa, kama wadau wanaotekeleza sheria ya mtoto ya mwaka 2009,inayosisitiza ulinzi na usalama wa mtoto,wameelekeza kuzingitiwa kwa sheria hiyo.

Ametaja miongoni mwa sababu zinazochangia changamoto,ni mwingiliano wa jamii,kutokana na kupakana na nchi mbalimbali,ambapo ni rahisi kufuata tamaduni tofauti na zinazo kinzana na maadili ya kitanzania.Hivyo Mkoa huo, unaendelea na juhudi za kupinga ukatili dhidi ya watoto pamoja na kusimamia sheria.