September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

LSF yatoa ruzuku bil.3.1/-kuongeza upatikanaji haki

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

SHIRIKA la Legal Services Facility (LSF) limetoa ruzuku yenye thamani ya shilingi za kitanzania bilioni 3.1 na wadau wake nchini, ambao ni mashirika nufaika ya wasaidizi wa kisheria, mashirika simamizi kwenye kanda sita, pamoja na mashirika mengine yanayotekeleza miradi kwenye maeneo muhimu ya kijamii (Thematic areas) hasa uchumi kwa ajili ya uwezeshaji kisheria kwa wananchi ikiwemo wanawake na watoto.

Sehemu ya ruzuku hii imetolewa kwa mashirika sita yatakayosimamia mashirika takribani 92 ya wasaidizi wa kisheria katika kanda sita nchini ili kuongeza ubora, uwezo, na maendeleo ya kitaasisi katika kutoa huduma bora za msaada wa kisheria kwa mwaka 2023.

Aidha, ruzuku yenye thamani ya shilingi bilioni 2.08 imetolewa moja kwa moja kwa mashirika 184 ya watoa huduma za msaada wa kisheria pamoja na wasaidizi wa kisheria nchi nzima Tanzania bara na Zanzibar kwenye kila ngazi ya mkoa na wilaya zote kwa ajili kukuza upatikanaji wa haki kwa wananchi kupitia utoaji wa huduma za msaada wa kisheria bure.

Akiongea kuhusu ruzuku hizo na matokeo yanayotegemea kupatikana, Mkurugenzi Mtendaji wa LSF, Lulu Ng’wanakilala amesema, “Ruzuku inayotolewa kwa mashirika ya watoa huduma za msaada wa kisheria na wasaidizi wa kisheria inakwenda kuchochea pia utekelezaji mkakati wa kamapeni ya huduma ya msaada wa kisheria ya mama Samia uliojikita kutoa msaada wa kisheria kwa wanawake na watoto kwa kutoa elimu katika jamii kuhusu haki za biandamu.

“Pia kupambana na ukatili wa kijinsia, utatuzi wa migogoro ya ardhi, masuala ya mirathi, kuelimisha wananchi kuhusu mifumo ya sheria, utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala pamoja na kujenga uwezo miongoni mwa wadau wa sekta ya msaada ya kisheria nchini” alisema.

Hali kadhalika,sehemu ya ruzuku hii imetolewa kwa Shirika la Kilimanjaro Women Information Exchange and Community Organization (KWIECO) kwa ajili ya kutekeleza mradi kwenye eneo la utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala ya usuluhishi (Altenative Dispute Resolution – ADR).

Mfumo wa utatuzi wa migogo kwa njia ya usuluhishi umeainishwa katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Ibara ya 107A(1)(d), ambayo inasisitiza kukuza na kuendeleza usuluhishi baina ya wanaohusika katika migogoro.

Kuwepo kwa mfumo huu wa utatuzi wa migogoro kutawawezesha wananchi hususani wanawake na watoto kupata haki zao kwa wakati katika ngazi ya awali ya utatuzi wa migogoro.

Vilevile, sehemu nyingine ya ruzuku imetolewa na LSF kwa mashirika matatu kwa ajili ya kutekeleza miradi katika maeneo maalumu ya kiuchumi yaani ‘Thematic Areas’ kwenye sekta ya kilimo, madini, na uchumi wa bahari kwenye mikoa ya Manyara na Lindi kupitia taasisi tatu za Community Support Initiatives Tanzania (COSITA), Lindi Association of Non-Governmental Organizations (LANGO), na Civic Social Protection Foundation (CSP).

LSF kwa kushirikiana na COSITA itawezesha wanawake kupata fursa zitokanazo na mazao ya kilimo pamoja na kilimo chenyewe kwa kuwajengea uwezo pamoja na kuondoa vikwazo vya kijamii katika masuala ya umiliki wa ardhi ili kuwawezesha kufanya kilimo chenye tija na kuongeza mnyororo wa thamani katika kilimo wilayani Babati.

Aidha, LSF kwa kushirikiana LANGO itaboresha maisha ya wanawake waishio maeneo ya mwambao wa bahari kupitia rasilimali bahari hasa mwani na tango bahari, ambayo ni mazao ya kibiashara yanayozalishwa zaidi na wanawake wengi pembezoni mwa bahari Mkoani Lindi.

Na eneo la mwisho la ruzuku hii, LSF kwa kushirikiana na CSP itatekeleza mradi unaojulikana kama ‘Tanzanite Kwa Uchumi Imara wa Mwanamke’ mradi ambao unalenga kuboresha mazingira ya wanawake wajasiriamali kufanya biashara pamoja kupunguza vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake kwenye mgodi wa Mirerani Mkoani Manyara.

Mkurugenzi Mtendaji wa Legal Services Facility (LSF), Lulu Ng’wanakilala