October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais wa Chama cha Walimu Tanzania.Leah Ulaya

Leah Ulaya aibuka kidedea urais CWT, Seif naye aula tena

Na Joyce Kasiki, TimesMajira Online, Dodoma

ALIYEKUWA Rais wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT ) Leah Ulaya amechaguliwa kwa mara nyingine tena kuwa Rais wa Chama hicho katika uchaguzi uliofanyika jana jijini Dodoma huku Deus Seif akichaguliwa tena kuwa Katibu Mkuu wa chama hicho.

Zoezi la upigaji kura lilianza jana Juni 5 saa tisa alasiri na matokeo kutangazwa na Mwenyekiti wa Uchaguzi, Suleiman Ikombo leo saa 11:30 alfajiri. Aliyekuwa Rais wa Chama cha Waalimu Tanzania, Leah Ulaya alipata kura 475 huku mpinzani wake akipata kura 365 kati ya kura 840 zilizopigwa.

Pia Ikombo alimtangaza Deus Seif kuwa Katibu Mkuu baada ya kupata kura 491 kati ya kura 869 zilizopigwa. Viongozi wengine waliochaguliwa ni pamoja na Makamu wa Rais Dinah Mathaman ambaye amepata kura 428 na kumshinda aliyekuwa akitetea kiti hicho Christopher Banda ambaye amepata kura 375 kati ya kura 869 zilizopigwa huku Naibu Katibu Mkuu alichaguliwa ni Maganga Japhet na Alawi Abubakari akichaguliwa kuwa Mweka Hazina ambaye amepata kura 534 kati ya kura 857 zilizopigwa.

Katika nafasi ya udhamini wa chama waliochaguliwa ni Faustine Salala, Emmanuel Aloyce na Clement Mswanyama huku Philipo Mahewa akichaguliwa kuwa Mjumbe wa TUCTA na Evodius Heneriko akichaguliwa kuwakilisha kundi la walimu vijana.

Wajumbe hao pia wamemchagua Shani Ulumbi kuwakilisha walemavu na Eliza Werema akiwakilisha wanawake.