
Na Joyce Kasiki – TimesMajira Online
KATIKA kipindi cha miaka saba tangu kuanzishwa kwake mwaka 2018, Kituo cha Utafiti wa Kilimo cha TARI Kihinga mkoani Kigoma kimepiga hatua kubwa katika kubadilisha taswira ya kilimo cha michikichi nchini, hasa kupitia uzalishaji wa mbegu bora aina ya Tenera na utoaji wa elimu kwa wakulima na maofisa ugani.
Akizungumza kwenye Maonyesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara Sabasaba, Mkurugenzi wa kituo hicho, Dkt. Wilson Kagimbo, amesema mafanikio yaliyopatikana ni matokeo ya juhudi za Serikali na ushirikiano mzuri na wadau wa maendeleo wa sekta ya kilimo.
Amesema ,tangu kuanza kwa uzalishaji wa mbegu mwaka 2018, kituo hicho kimezalisha jumla ya mbegu milioni 18.59, ambapo kati ya hizo miche milioni 4.69 imepatikana, na miche milioni 3.48 tayari imepandwa kwenye mashamba mbalimbali nchini, ikihusisha jumla ya hekta 27,908 zilizopandwa michikichi ya kisasa.
Dkt. Kagimbo ameeleza kuwa mafanikio hayo yamepunguza utegemezi wa mbegu kutoka nje ya nchi, hatua iliyosaidia kuokoa fedha nyingi za kigeni.
“Kabla ya kuanzishwa kwa kituo hiki, mbegu bora za michikichi zilikuwa zinaagizwa kutoka nje kwa gharama kubwa, ambapo mche mmoja uliuzwa kati ya Sh 6,000 hadi 15,000. Tangu Serikali ilipoamua kutoa kipaumbele kwa zao hili, tumeweza kuzalisha na kugawa bure miche kwa wakulima. Kama mbegu hizo zingekuwa zimenunuliwa kutoka nje, zingetugharimu zaidi ya Sh bilioni 18.7,” amesema Dkt. Kagimbo.
Pamoja na kazi ya uzalishaji mbegu, kituo hiki pia kimejikita katika kutoa elimu ya kilimo bora cha michikichi kwa wakulima na maofisa ugani. Hadi kufikia Julai 2025, wakulima 2,266 na maofisa ugani 276 wamepatiwa mafunzo maalum. Aidha, wanafunzi 96 kutoka vyuo vya kati na vyuo vikuu pamoja na wanafunzi 214 wa sekondari wamepatiwa mafunzo ya vitendo, jambo linalosaidia kuandaa wataalamu wa baadaye wa zao hilo.
Moja ya changamoto kubwa iliyokuwepo kabla ya 2018 ilikuwa ni ukosefu wa elimu ya kilimo cha kisasa cha michikichi, kwani zao hilo halikupatiwa kipaumbele katika mitaala ya vyuo vya kilimo. Tangu Serikali ilipoliweka katika orodha ya mazao ya kimkakati, elimu imeanza kutolewa rasmi vyuoni, huku kituo cha Kihinga kikiwa kiungo muhimu katika mabadiliko hayo.
Katika juhudi za kuhamasisha uwekezaji katika zao la michikichi, TARI Kihinga pia imefanya kazi kubwa kupitia vyombo vya habari ambapo mpaka sasa, kituo kimerekodi na kurusha vipindi 88 vya televisheni, 60 vya redio, na kuchapisha zaidi ya makala 180 katika magazeti na blog mbalimbali, vikielezea faida za kilimo cha kisasa cha michikichi na fursa za uwekezaji kwenye mnyororo wa thamani wa zao hilo.
Dkt. Kagimbo amebainisha kuwa, wakati kituo kinaanza kazi, michikichi ya kienyeji aina ya Dura ilikuwa inapatikana kwa asilimia 90, huku aina bora ya Tenera ikipatikana kwa asilimia tisa tu. Kupitia kazi ya kituo hicho, mwelekeo sasa umebadilika na wakulima wengi wameanza kuelewa faida ya kutumia mbegu bora kwa ajili ya tija zaidi.
Akizungumza namna TARI inavyoweza kusaidia upatikanaji wa mafuta ya kula nchini amesema,mahitaji ya mafuta ya kula nchini ni takriban tani 650,000 kwa mwaka, na kupitia mkakati wa kuongeza uzalishaji wa michikichi, TARI Kihinga inalenga kusaidia nchi kujitosheleza.
“Kwa sasa, ili kufikia uzalishaji wa mafuta yanayohitajika nchini, inakadiriwa kuwa zinahitajika hektari 1,062,500 za michikichi,kwa miche iliyokwisha pandwa, nchi imefikia hektari 27,908, na matarajio ni kuongeza kasi zaidi katika miaka mitatu hadi minne ijayo.”amesisitiza
Dkt. Kagimbo amesema kuwa mafanikio haya ni matokeo ya maamuzi sahihi ya Serikali katika kukipa kipaumbele kilimo cha michikichi na uwekezaji katika utafiti.
“Tunajivunia kuwa sehemu ya suluhisho la upungufu wa mafuta ya kula nchini,na kwa kasi tuliyo nayo, tunaamini Tanzania inaweza kujitegemea katika miaka michache ijayo,” amesema.

More Stories
Wanawake jumuia ya kikristo Tanzania CCT wafundana kuelekea siku ya Wanawake Duniani
Dkt.Tulia,Mwalunenge waungana kutatua changamoto ya barabara
TUCASA yaomba kuanzishwa sheria malipo sekta ya ujenzi