September 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kata ya Kimanga kujengwa upya,kuwa ya kisasa

Na Heri Shaaban, Timesmajira Online,Ilala
MBUNGE wa Jimbo la Segerea Bonnah Kamoli amesema Kata ya Kimanga inatarajia kujengwa upya kuwa ya kisasa kwani serikali inaelekeza maendeleo katika kata hiyo kwa kujenga barabara za kisasa, masoko na kituo cha daladala cha kisasa.

Bonnah amesema hayo katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kata ya Kimanga Jimbo la Segerea wilayani Ilala mkoani Dar-es-Salaam.

“Kata ya Kimanga imekaa muda mrefu bila kupata maendeleo kutokana na awali kuongozwa na CHADEMA 2015 kwa sasa kata hiyo inaongozwa CCM hivyo wananchi watoe ushirikiano kwa ajili ya maendeleo kwa sasa naweka kambi maalum katika kata hii kwa ajili ya kufuatilia maendeleo yote yafanyike haraka,”amesema Bonnah.

Amesema barabara za kisasa za ndani zitajengwa na mradi wa DMDP hivi karibuni ikiwemo za Savannah, Mwananchi ,Tabata, Kisiwani,Bima Mazida Maboresho,Barakuda Tabata Chang’ombe mpaka mMaji Chumvi zitajengwa kwa kiwango cha lami.

Kwa upande wa vivuko vitakavyo jengwa na Serikali ni kivuko cha Mzawa ambapo kitaunganisha mawasiliano ya Liwiti na Kimanga na kivuko cha Kasevu.

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kata ya Kimanga George Mtasingwa,amesema katika kata hiyo serikali inatarajia kujenga shule nyingine ya sekondari hivi karibuni baada eneo kupatikana hivyo changamoto zinazoikabili zitakwisha ambapo eneo la kituo cha zahanati limepatikana mchakato wa ujenzi umeanza soko linatarajia kujengwa kwa ajili ya fursa kwa wananchi wa Kimanga.

Diwani wa Viti Maalum Wanawake Wilaya ya Ilala Rukia Mwenge alizungumzia mikopo ya Serikali inayotolewa ngazi ya Halmashauri ya asilimia kumi amesema Kimanga jumla ya vikundi 92 vimeomba mikopo na vikundi vilivyopewa fedha hizo ni vikundi 53 jumla ya Fedha walizokopa milioni 400.