March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kampeni ya Polio kuwafikia watoto Mwanza

Judith Ferdinand, Timesmajira Online-Mwanza

Serikali kupitia Wizara ya Afya inatarajia kufanya kampeni maalumu ya chanjo ya matone dhidi ya ugonjwa wa polio kwa watoto wenye umri chini ya miaka 10,katika mikoa saba itakayofanyika kwa siku nne kuanzia Machi 24 hadi 27 mwaka huu.

Kampeni hiyo ni sehemu ya mpango wa kitaifa utakaotekelezwa katika mikoa saba ambayo ni Mwanza, Simiyu, Shinyanga, Mara, Singida, Geita na Tabora kwa lengo la kuimarisha kinga ya watoto dhidi ya ugonjwa huo hatari.

Akizungumza na Majira Machi 4, 2026, Kaimu Mratibu wa Chanjo Mkoa wa Mwanza, Sia Urassa,amesema,katika kampeni hiyo Mkoa wa Mwanza,unatarajia kuchanja takribani watoto milioni 1.2 wenye umri wa chini ya miaka 10 dhidi ya ugonjwa wa polio.

Ambapo amewahimiza wazazi na wananchi kwa ujumla kujitokeza kwa wingi na kuhakikisha watoto wao wanapatiwa chanjo hiyo katika kampeni hiyo kwa kuwa ni salama, muhimu na inatolewa bure.

Urassa amesisitiza kuwa watoto wote wenye umri chini ya miaka 10 watapata chanjo hizo hata kama aliishapata dozi awali,kwani ugonjwa wa polio ni hatari unaweza kusababisha ulemavu wa kudumu kwa mtoto endapo hatapata chanjo kwa wakati.

“Mtoto anapopata ulemavu wa kudumu, mzazi hulazimika kutumia muda mwingi kumhudumia na kushindwa kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na uzalishaji mali, jambo linaloweza kuongeza umasikini katika familia,”amesema Urassa.

Urassa amesema,kupitia kampeni hiyo chanjo hiyo itatolewa katika vituo vya kutolea huduma za afya, nyumba kwa nyumba na katika shule za msingi,chekechea na vituo vya kuleta watoto mchana( day care), ili kuhakikisha watoto wote wanafikiwa kwa urahisi.

Pia amesema,kutakuwa na timu maalumu zitakazofanya kazi katika maeneo magumu kufikika ikiwemo kufuata wavuvi katika maeneo yao ili kuhakikisha hakuna mtoto anayekosa chanjo katika kipindi cha kampeni.

Amesema Wizara ya Afya tayari imepeleka chanjo za kutosha pamoja na vifaa vyote vinavyohitajika kwa ajili ya kufanikisha zoezi hilo mkoani Mwanza.