Na Mwandishi wetu, Timesmajira
Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida imezindua rasmi Kamati ya Ushauri wa Kisheria ngazi ya Mkoa na Wilaya na Kliniki ya Sheria bila malipo kwa Wananchi wa Mkoa wa Singida.
Uzinduzi huo umefanyika leo tarehe 19 Mei, 2025 katika viwanja vya Stendi ya zamani Manispaa ya Singida na Mkuu wa Mkoa huo, Halima Dendego ameipongeza Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuuchagua Mkoa wa Singida na kuja kuzindua Kamati ya Ushauri wa Kisheria ngazi ya Mkoa na Wilaya kwa kuwa ni fursa kwa wananchi wa mkoa huo kutatuliwa changamoto mbalimbali za kisheria zinazowakabili.
“Kipekee naishukuru Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Kamati ya Ushauri wa Kisheria ngazi ya Mkoa na Wilaya kwa kunifikiria na kunipa wajibu huu mkubwa wa kuwa Mgeni Rasmi katika Halfa hii ya Uzinduzi wa Kamati na Kliniki ya Sheria bila malipo katika mkoa wetu”. amesema Dendego.
Dendego amesema kuwa kuzinduliwa kwa Kamati hiyo pamoja na masuala mengine, kutasaidia kupunguza mashauri au migogoro dhidi ya Serikali, Kuwawezesha Mawakili wa Serikali kusimamia Utawala wa Sheria katika maeneo yao, Kuwawezesha Mawakili wa Serikali kushirikiana na wadau wengine katika kutatua kero za wananchi na kupunguza malalamiko ya kisheria kutoka kwa wananchi.

“Naomba kukuahidi Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuwa nitazisimamia Kamati hizi kikamilifu ili ziweze kuwa na tija katika mkoa wetu.”amesema Dendego
Katia hatua nyingine Mkuu wa Mkoa wa Singida ametoa wito kwa Wananchi wa Mkoa huo kujitokeza kwa wingi katika Kliniki ya Sheria bila malipo ili waweze kupata huduma mbalimbali za kisheria hususani katika masuala ya mirathi, Ardhi, ndoa na Ajira.

“Nitoe wito kwa Wananchi wa Singida kujitokeza kwa wingi katika Kliniki hii kwani Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imekuja na Wataalamu waliobobea katika masuala ya Kisheria na wanatoa huduma hii bure kabisa.” Amesema Dendego

Kwa upande wake Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Hamza Johari amesema kuwa kuzinduliwa kwa Kamati ya Ushauri wa Kisheria ngazi ya Mkoa na Wilaya pamoja na Kliniki ya Sheria kwa Wananchi wa Mkoa wa Singida ni mojawapo ya hatua za Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika kusogeza huduma za kisheria karibu zaidi na wananchi.
Aidha, Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameeleza kuwa moja ya njia inayotumiwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuwajibika kwa wananchi ni kutoa ushauri na msaada wa kisheria kwa wananchi kwa kutumia Kamati za Ushauri wa Kisheria kwa ngazi ya Mkoa na ngazi za Wilaya.

“Lengo kuu la uanzishwaji wa Kamati za Ushauri wa Kisheria kwa ngazi ya Mkoa na Wilaya ni kurahisisha usimamizi wa utoaji wa ushauri wa kisheria kwa wananchi katika maeneo husika”. Amesema Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali amesema kuwa, Uzinduzi wa Kamati ya Ushauri wa Kisheria kwa Mkoa wa Singida utafuatiwa na Kliniki ya sheria kuanzia Mei 19 hadi 25, 2025 ambapo huduma za ushauri wa kisheria zitatolewa kwa wananchi bila malipo, ambapo amesisitiza Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali itatoa huduma hizo kwa ubora.“Tunawaahidi tutatoa huduma hii bila malipo kwa wananchi na kwa weledi mkubwa”. Amesema Mwanasheria Mkuu wa Serikali
Vilevile, Johari amesema kuwa Kliniki hiyo ya Sheria inalenga kusogeza huduma za sheria karibu na wananchi, kuwaongoza wananchi katika taratibu za kupata haki zao pale zinapovunjwa au zinapoonekana kuelekea kuvunjwa, kutoa elimu ya sheria kwa wananchi na kuongeza ushirikiano miongoni mwa Mawakili wa Serikali na Mawakili wa Kujitegemea, na kuepusha au kupunguza mashauri yasiyo ya lazima.
“Kupitia huduma zitakazotolewa kwenye Kliniki hii ya Sheria tunaamini tutaongeza utengamano na utulivu katika jamii, kudumisha utawala bora kwa kuimarisha utawala wa sheria nchini, na kuchochea maendeleo kwa jamii na taifa kwa ujumla”. Amesema Johari.
More Stories
Kongamano la kimataifa la kusoma Qur’an kufanyika Mei 24,2025
KUTAMBUA WAHALIFU WANAOTUMIA MITANDAO YAKO YA KIJAMII BILA RIDHAA YAKO
Nafasi ya Tokeni ya Uthibitisho katika Usalama wa Mtandao